NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha Sauti ya Umma (SAU) kimesema Serikali yake haitaruhusu wenye nyumba kujaza frame za maduka ya biashara katika maeneo ya makazi
Hata hivyo Serikali ya SAU itatenga sehemu maalum na kujenga barabara zitakazotumika kwa ajili ya biashara.
Kwa mujibu wa Ilani ya Chama hicho yenya kauli mbinu Amani,Uadilifu na Maendeleo iliyopitishwa April 28,2025 yenye nguzo muhimu za Kilimo, Viwanda na Teknolojia inaeleza kuwa ni Ilani ya ukombozi kwa mtanzania ambapo juu ya nguzo hizo SAU inakwenda kuboresha maisha ya watanzania na maendeleo ya taifa.
“Ilani hii ni mtiririko wa ahadi za chama kwa wapiga kura na watanzania wote, inaonyesha dira, maadili, sera na mipango ya chama katika kipindi cha miaka mitano ya utawala na kwa jinsi gani tutaweza”imefafanuwa Ilani hiyo
Kwa upande wa masuala ya ardhi,SAU imebainisha kuwa upimajiwa ardhi umesuasua na kupelekea kutokea dhuluma na kesi nyingi ambazo hazikupaswa kutokea ambapo wakati mwingine watendaji wa wizara husika wanakuwa chanzo cha gomvi hizo.
“Chama cha SAU kupitia Serikali yake kitahakikisha kila ardhi ya Tanzania inapimwa, inamilikishwa na kulipiwa kodi. Hii itaondoa ugomvi na kuongeza pato kwa taifa na wale ambao hawana matumizi ya ardhi hawatakubali kukaanayo pasipo izalisha.
“Kurekebisha wizara ya ardhi na kuweka wafanyakazi waadilifu ili kuondoa malalamiko na dhuluma za ardhi kwa wananchi mbalimbali”imeongeza Ilani hiyo
Ilani hiyo imeeleza kuwa Serikali ya SAU itatumia vyema ardhi kubwa iliyopo kwa kuhusisha wawekezaji wakubwa wa ndani na nje ya nchi, katika kilimo na viwanda ili ajira nyingi zaidi zipatikane na uuzaji mkubwa wa bidhaa nje ya nchi.
“Kodi ya majengo kwa nyumba za makazi itafutwa kabisa na kutokuruhusu ujenzi wa maduka ya biashara katika maeneo ya makazi.
“Sehemu na barabara maalumu zitatengwa badala ya kila mwenye nyumba kujaza frame za maduka mbele ya nyumba yake.
“Vikundi vya kina mama vicoba vitapewa ardhi bure ili wawekeze katika kilimo, ufugaji, uvuvi, majengo kama hostel n.k na kupunguza gharama za vifaa vya ujenzi”imebainisha Ilani hiyo
Ilani hiyo imeonesha kuwa Serikali ya SAU itajenga nyumba bora za gharama nafuu 200,000 za makazi vijijini ambazo zitajengwa katika kipindi cha miaka mitano, kwa kushirikiana na Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Sekta binafsi, taasisi za fedha na viwanda vya vifaa vya ujenzi.
“Tutaanzishwa kampeni maalum vijijini ya nipe mazao au mfugo nikupe nyumba bora katika eneo lako. Lengo ni kuhakikisha watanzania wanaishi maisha bora”imeeleza Ilani hiyo
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho Betha Mpata amesema Ilani imefafanua ni jinsi gani Chama cha Sauti ya Umma kitakavyo mhudumia mtanzania endapo atakipa mamlaka ya kushika dola kwa kuwapa wagombea wake kura nyingi za ndio katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2025.
“Kama Mwenyekiti wa Chama cha Sauti ya Umma (SAU), pamoja na viongozi wenzangu wa chama chetu, tunayo dhamira ya dhati ya kuleta mabadiliko na maendeleo na kujenga mustakabali mzuri kwa wote.
“Sambamba na kulinda muungano wetu na kukuza umoja na mshikamano miongoni mwa watanzania na waafrika.
“Ilani hii ni zaidi ya hati ni ahadi, ahadi ya kupigania haki zako na kufanya kazi bila kuchoka ili kuunda jamii yenye haki, jamii yenye maendeleo na jumuishi.”amesema Mpata
Hata hivyo Mpata amebanisha kuwa Ilani yao ni ramani ya mabadiliko wanayoyahitaji kwa pamoja na kupitia SAU wanaweza kushinda changamoto za leo na kujenga kesho iliyobora ambayo wote wanaweza kujivunia.
“Rai yangu, ninawaomba sana muungane nasi na mchukue maamuzi sahihi ya kuiamini na kuichagua kwa kura nyingi Chama cha Sauti ya Umma (SAU) ili kupata mustakabali bora kwa ajili yetu na kwa vizazi vijavyo”ameongeza Mpata
Katibu Mkuu wa SAU na Mgombea wa nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Majalio Kyara amesema amekuja kwa watanzania si tu kama mgombea Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia kama mtanzania anayeelewa changamoto zinazowakabili na kesho wanayoitamani.
“Nchi yetu imebarikiwa kuwa na ardhi yenye rutuba, rasilimali nyingi na idadi nzuri ya vijana wanaotaka kuchangia maendeleo yetu ya pamoja.
“Hata hivyo, hatuwezi kupuuza hali halisi ya umaskini, ukosefu wa ajira na miundombinu duni ambayo inazuia ukuaji wetu.
“Nguzo zetu kuu za Kilimo, Viwanda na Teknolojia katika Ilani hii ya 2025 – 2030, zitawezesha kusukuma maendeleo, kudumisha jamii zetu, upatikanaji wa ajira na maendeleo kwa vijana wetu”amebainisha Kyra
Kayra ameongeza kuwa wanatazamia Taifa ambalo hakuna aliyesalia nyuma ambapo ndoto za vijana, hekima za wazee, na bidii za wakulima, wafanyakazi na wajasiriamali zinauungwa mkono.
Watanzania wanatarajiwa kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025 na kuwachagua wagombea wa nafasi ya Urais,Ubunge na Udiwani watakaodumu kwa muda wa miaka mitano hadi 2030 utakapoitishwa uchaguzi mwingine.



Discussion about this post