NA GOODLUCK HONGO
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles Kichere amebainisha kuwa katika mradi wa Dege Eco Village ardhi yenye ukubwa wa kilometa za mraba 92,770.39 ilikuwa imevamiwa kinyume cha sheria ikiwa na thamani ya Sh. Bilioni 1.41.
Dege Eco Village ni mradi uliotekelezwa kupitia mkataba wa ubia kati ya Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi na Kampuni ya Nyumba ya Azimio.
Mkataba huu uliositishwa Machi 2016 kufuatia masuala ya udhibiti yaliyotolewa na Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii na Benki Kuu ya Tanzania.
CAG Kichere ameyasema hayo katika Ripoti Kuu ya Mwaka ya Ukaguzi wa Mashirika ya Umma wa Mwaka wa Fedha 2024/2025 iliyotolewa tarahe30/3/2026.

Aidha, amebaini kuwa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi, kupitia Mthamini wa Serikali, umebaini thamani ya ardhi iliyovamiwa kuwa ni dola za Marekani 547,044.50 (sawa na shilingi bilioni 1.41).
Amesema udhaifu huo ulisababishwa zaidi na usimamizi duni na ufuatiliaji usioridhisha wa sehemu hiyo ya ardhi ambapo Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi ulieleza kuwa unashirikiana na Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni kurejesha mpaka wa sehemu ya ardhi iliyovamiwa.
“Majadiliano pia yanaendelea kwa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi kukutana na viongozi wa serikali za mitaa, huku ajenda ikiwa sehemu ya ardhi iliyovamiwa.
“Kwa maoni yangu, ikiwa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi haitatumia haki yake ya umiliki wa ardhi hiyo, kuna uwezekano mkubwa wa kupoteza sehemu ya ardhi iliyovamiwa, ambayo hatimaye itasababisha hasara kwa Mfuko.
“Ninapendekeza kuwa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii kwa Sekta Binafsi uharakishe mchakato wa uwekaji mipaka halisi ya ardhi iliyovamiwa na kuirejesha ardhi yote iliyovamiwa kwa gharama ya wavamizi”ameeleza CAG Kichere

Discussion about this post