NA GOODLUCK HONGO
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles Kichere amesema ucheleweshaji wa kuhamisha mashine na vifaa vya Kiwanda cha Urafiki kilichopo mkoani Dar es Salaam yamesababisha Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) upotevu wa mapato ya Sh.Bilioni 3.36 kwa mwaka wa fedha 2024/25.
Amesema mnamo tarehe 03 Novemba 2023, Shirika la Nyumba la Taifa lilishiriki na kushinda mnada wa kununua mali zilizokuwa zinamilikiwa na Kiwanda cha Urafiki (Lot 1, Kitalu Na. 409, Kiwanja Na. 1 pamoja na viwanja mbalimbali vya nyumba za wafanyakazi) kwa bei ya Sh.Bilioni 3.60 katika mnada ulioendeshwa kwa amri ya mahakama kupitia Kampuni ya Santana iliyoteuliwa na mahakama.

CAG Kichere ameyabainisha hayo katika Ripoti Kuu ya Mwaka ya Ukaguzi wa Mashirika ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 iliyotolewa tarehe 30/3/2026 .
“Mapitio yangu ya uwekezaji wa Shirika la Nyumba la Taifa katika eneo la Urafiki kwa mwaka ulioishia tarehe 30 Juni 2025, ambayo yalijumuisha ziara yangu katika eneo la uwekezaji uliofanyika tarehe 14 Novemba 2025, yalibaini kuwa mojawapo ya mali zilizonunuliwa na Shirika ni jengo ambalo kwa sasa linahifadhi mashine za Kiwanda cha Urafiki ambazo hazikua sehemu ya mali zilizonunuliwa na zinatakiwa kuondolewa na wamiliki wa Kiwanda cha Urafiki.
“Jengo hili lenye mita za mraba 35,019.69 linaweza kukodishwa kwa bei ya soko ya Sh. 8,000 kwa mita ya mraba, hivyo kuzalishia Shirika mapato ya Sh.Milioni 280.15 yatokanayo na kodi kwa mwezi.
“Ucheleweshaji wa kuhamisha mashine na vifaa vya Kiwanda cha Urafiki yamesababisha Shirika la Nyumba la Taifa kushindwa kukodisha eneo hilo; hivyo kusababisha upotevu wa mapato ya Sh.Bilioni 3.36 kwa mwaka wa fedha 2024/25″amesema CAG Kichere.

Hata hivyo CAG Kichere amependekeza kuwa Shirika la Nyumba la Taifa lifuatilie kwa ukaribu pande zinazohusika kukamilisha mazungumzo ili kuharakisha uhamisho wa mashine na vifaa vya kiwanda cha Urafiki.
Aidha ameongeza kuwa hiyo itawezesha kukodishwa kwa maeneo ambayo kwa sasa yapo chini ya kizuizi na kuliongezea Shirika mapato.

Discussion about this post