Na Mwandishi Wetu,MOROGORO
WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kujikita katika kuandika habari za mazingira ili kuunga mkono jitihada za serikali za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwa faida ya kizazi cha sasa na kijacho.
Wito huo ulitolewa na Mkuu wa Chuo cha Misitu,Wanyamapori na Utalii katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA)Prof. Suzana Augustino wakati akizungumza na waandishi wa habari za mazingira (JET) mkoani Morogoro juu ya biashara ya kaboni.
Amesema Tanzania ni nchi mwanachama wa Mpango wa Umoja wa Mataifa wa kuthibiti mabadiliko ya tabianchi (UNFCCC) ulioanzishwa mwaka 1992.
Amesema mpango huu unatoa wito kwa nchi wanachama kupunguza Gesi Joto (GHGs) katika anga ambazo ndizo sababu ya mabadiliko ya tabianchi.
“Athari za mabadiliko tabianchi ni pamoja na kuongezeka kwa ukame na mafuriko ya mara kwa mara, uhaba wa chakula na maji, kuenea kwa magonjwa ya kuambukiza kama Malaria na Homa ya Bonde la Ufa (RVF), kuyeyuka kwa seruji kwenye milima mirefu na kwenye ncha za Dunia na vile vile kutoweka kwa visiwa vidogo”amesema Prof.Augustino
Aidha amefafanua kuwa kuna juhudi za kitaifa na kimataifa za kushughulikia mabadiliko ya Tabianchi na mojawapo ni ni biashara ya kaboni (hewa ukaa).
Ameongeza kuwa biashara ya kaboni ya misitu ilikuwa inawezekana tu kupitia sera ya maendeleo safi (CDM) ya Itifaki ya Kyoto ya UNFCCC ambapo shughuli za upandaji miti mipya zinaruhusiwa.
“Licha ya kuwa na eneo kubwa la misitu, Tanzania haikupata miradi ya CDM ya kupanda miti chini ya Itifaki ya Kyoto kwa sababu ya ukosefu wa utaalam na teknolojia.”
“Mtu akiona misitu ajue ameona hela na mtu anatunza miti ili kupata fedha hivyo hii nayo ni fursa ya kuuza Kaboni na ndio maana serikali iliamua kuanzisha pia Kituo cha Kitaifa cha Kufuatilia Kaboni”amesema Prof.Augustino.
Akifafanua kuhusu soko la Kaboni,Mkurugenzi wa Kituo cha Kitaifa cha Kufuatilia Kaboni (NCMC) Prof.Eliakim Zahabu amesema katika soko huria la Kaboni kuna sehemu mbili ambapo moja ni makampuni binafsi kuwekeza kwenye kufyonza gesi joto na ya pili ni Nchi inafuata vigezo vya Mpango wa Umoja wa Mataifa wa Kudhibiti Mabadiliko ya Hali ya Hewa duniani (UNFCC).
“Ukiona mti umekuwa ujue umehifadhi kiwango kikubwa cha Kaboni na ukichoma misitu basi ujue kaboni inakwenda angani na kwa Tanzania matumizi ya kilimo ndio yameonekana kuzalisha Kaboni kwa wingi kutokana na watu kufyeka misitu na kuchoma moto ili kuandaa mashamba”amesema Prof.Zahabu
Prof.Zahabu amefafanua kuwa Nchi, Mashirika na Watu binafsi wanaweza kuanzisha shughuli za kupunguza kiwango cha hewa ukaa(Kaboni) kwa kupanda miti mipya.
“Soko rasmi la Kaboni ni kwa kupitia Mpango wa Umoja wa Mataifa wa Kudhibiti Mabadiliko ya Hali ya Hewa duniani (UNFCC) hususani Sera ya Maendeleo safi(CDM) ya Protokali ya Kyoto ambayo inaruhusu shughuli za upandaji wa miti mipya na kwa Tanzania mikoa inayofanya miradi ya Kaboni ni Mbeya,Katavi na Arusha”
“Shughuli zingine kama utunzaji shirikishi wa misitu ya jamii (CFM) nchini unaohusisha misitu asilia ambayo ingetoweka ama kuharibika na kutoa hewa ukaa(Kaboni) inaweza pia kupata malipo kupitia Mpango wa Kupunguza Uzalishaji wa Hewa Ukaa kutokana na ukataji miti hovyo na uharibifu wa misitu”amesema Prof.Zahabu
Kwa upande wake Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha SUA Dkt.Deo Shirima amesema kila kitu kinachofanyika lazima kichangie asilimia kadhaa ya fedha ili kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi kwa kuwa hata ukipanda ndege unachangia pia hewa ukaa.
Akizungumza kwa niaba ya waandishi wa habari,Mkurugenzi wa JET John Chikomo amesema JET itaendelea kuhakikisha kuwa wandishi wa habari wanajikita zaidi katika kuandika habari za mazingira ili kusaidia nchi kwa vizazi vya sasa na vijavyo.
“Kulinda mazingira ni suala la kila mmoja wetu hivyo sisi kupitia vyombo vya habari tuna jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa mazingira yanalindwa kwa ajili ya sasa na vizazi vinavyo”amesema Chikomo
MWISHO
Discussion about this post