NA GOODLUCK HONGO
SERIKALI kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imeendelea kuwaibua wabunifu wa teknolojia mbalimbali nchini ambapo sasa imemsaidia Mtanzania Patrick Kitosi kuendeleza mashine aliyoibuni kuvunia sumu ya nyuki.
Hata hivyo mbunifu huyo amebainisha kuwa sumu ya nyuki mara nyingi inatumika katika matibabu ya magonjwa mbalimbali lakini ilikuwa vigumu kuivuna bila kuwaathiri nyuki na shughuli zao za kila siku katika uzalishaji wa asali na kulinda mazingira.
Akizungumza jijini Dar es Salaam Machi 8,2023 wakati wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kati ya waandishi wa Habari na Watafiti yaliyoandaliwa na COSTECH,Kitosi amesema alianza kufanya utafiti wa mashine hiyo mwaka 2017 na kufanya majaribio 16 kabla ya kufanikiwa kuwa na mashine ambayo huvuna sumu ya nyuki bila kuwaathiri.
Amesema nyuki wapo wa aina tofauti kulingana na mazingira na nchi wanakotoka yakiwemo ya joto na baridi hivyo teknolojia ya mashine yake lazima izingatie hali hiyo ili wasiweze kudhurika ikiwemo kuuawa na kukatika mikia wakati zoezi la uvunaji wa sumu hiyo ukifanyika .
“Ili nyuki atoe sumu lazima akasirike ambapo katika mkia wake anaotumia kung’ata unakuwa na majimaji ambayo ndio sumu yenyewe,sasa sisi mashine yetu tumetumia teknolojia ya eletroniki na umeme hivyo nyuki anapotua hupigwa shoti na hapo ndipo hukasirikika na kutoa sumu.
“Wakati anatoa sumu hiyo mkia wake hubakia bila kukatika tofauti aking’ata kawaida ambapo mkia wake hukatika,mashine pia inakuwa na kioo baada ya nyuki kung’ata waya zilizowapiga shoti ndipo majimaji hayo yenye sumu hudondoka kwenye kioo kwa uzito wa 0.6 gram kwa kutegemea na kundi la nyuki na huchukua dakika 30 kuvuna sumu hiyo “amesema Kitosi
Kitosi ameishukuru COSTECH kwa kuhakikisha kuwa ubunifu wake unaendelea kusaidia wafugaji wa nyuki bila kuathiri mazingira yao ambapo hadi sasa ameshauza mashine 107 nchini huku kila moja ikiwa na thamani ya Sh.750,000 ambapo mashine kama hiyo kutoka nje ya nchi inagharimu zaidi ya Sh.Milioni mbili.
“Licha ya Nyuki kutoa asali lakini pia sumu yake inauzwa bei ghali sana nje ya nchi lakini pia hutoa Nta na Maziwa na hiyo inatokana na vitu vyote wanavyovizalisha hutokana na mimea.
“Nyuki wanaakili sana lazima utafiti wa kina ufanyike ili kugundua mashine hiyo lakini changamato kubwa iliyopo ni wafugaji kutojua sumu ya nyuki kama inaweza kuuzwa na jinsi ya kuivuna ikiwemo uhaba wa mashine hizo za kuvunia”amebainisha Kitosi
Hata hivyo Kitosi ameongeza kuwa ubunifu wa mashine hiyo utasaidia katika upatikanaji wa madawa ya kutibu magonjwa mbalimbali na kupunguza gharama za matibabu.
Awali Mkurugenzi wa Menejimenti ya Maarifa kutoka COSTECH Mhandisi Samson Mwela amesema mtu yeyote mwenye bunifu yake anakaribishwa kuzipeleka COSTECH ili ziweze kuendelezwa na kutatua changamoto kwa jamii.
“Kazi ya Serikali ni kuweka mazingira mazuri ya Sayansi,Teknolojia katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi na kuleta maendeleo kwa Taifa letu”amesema Mhandishi Mwela




Discussion about this post