NA GOODLUCK HONGO
TAASISI ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) inatarajiwa kuzalisha miche 500,000 ya zao la Mkonge kwa kutumia teknolojia ya chupa kutokana na ongezeko la mahitaji yake kitaifa.
Mbali na hilo lakini pia taasisi hiyo inaendelea na uzalishaji wa miche bora ya zao la Nanasi ambalo hukaa muda mrefu bila kuharibika na lenye ubora wa kuuzwa nje ya nchi bila tatizo.
Uzalishaji wa miche hiyo unafanyika katika Kituo cha TARI-Mikocheni jijini Dar es Salaam ambapo Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH)imesaidia katika kuhakikisha kuwa teknolojia hiyo inasaidia Taifa kukabiliana na uhaba wa mbegu bora za mazao.
Akizungumza jijini Dar es Salaam Machi 8,2023 wakati wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kati ya waandishi wa Habari na Watafiti yaliyoandaliwa na COSTECH,Mtafiti kutoka TARI-Mikocheni Margareth Lupembe amesema mbegu hizo zote zinazalishwa kwa njia ya chupa ndani ya maabara.
Amesema wao wamekuwa wakitumia teknolojia hiyo ya chupa maarufu kama Tissue Culture kwa muda mrefu ambapo mmea huzalishwa ndani ya chupa iliyokuwa na virutubisho vyote vinavyosaidia mmea kukua kama unavyokuwa nje.
“TARI-Mikocheni inatakiwa kuzalisha miche ya Mkonge 500,000 ifikapo Julai mwaka huu kwa ufadhili wa serikali kupitia TARI Mlingano ili iweze kusambazwa kwa wakulima.
“TARI-Mikocheni sio tu tunazalisha miche ya Mkonge pekee au Nanasi lakini pia kuna mazao mengine kama migomba, mihogo na viazi vitamu ambayo yote tunazalisha kwa kutumia teknolojia ya chupa.”amesema Lupembe
Lupembe amefafanua kuwa uzalishaji wa mbegu bora kwa njia ya chupa ni tofauti na uzalishaji wa mbegu kwa njia zingine kama GMO hivyo ni muhimu wakulima na wadau wengine wa kilimo kujua hilo.
“Faida ya uzalishaji huu wa miche kwa njia ya chupa ni kwamba inatunza vinasaba,mimea yote inafafana kwa kuwa itatoka katika shina moja lakini pia ladha ni ile ile na mbegu zake zinaweza kupandwa kama kawaida”ameongeza Lupembe
Hata hivyo Lupembe amebainisha kuwa faida nyingine nikupunguza mahitaji ya uhaba wa mbegu kwa kuwa mbegu moja inatoa miche 200 kupitia uzalishaji wa njia ya chupa.
Awali akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Menejimenti ya Maarifa kutoka COSTECH Mhandisi Samson Mwela amesema Serikali inavipaumbe vyake vya mazao na wao kama Tume wameendelea na ufadhili wa mradi wa kuzalisha mbegu za Nanasi kwa njia ya chupa.
“Tunafanya tafiti za kisayansi ili kuleta mabadiliko kwa wananchi na kuwanufaisha hivyo vyombo vya habari mnawajibu wa kuwafikishia waananchi taarifa hizi kwa lugha itakayowasidia kuelewa kwa urahisi”amesema Mhandisi Mwela
Kwa upande wake Mratibu wa Mafunzo ya Uandishi wa Habari za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kutoka COSTECH Deusideth Leoanaed amesema hayo ni mafunzo ya tisa kufanyika tangu mwaka 2015 ya kuwakutanisha Waandishi wa Habari,Watafiti na Wabunifu.
“Lengo ni kuwaleta pamoja na kubadilishana uzoefu ili tafiti nyingi ziweze kuandikwa kwa lugha rahisi,kupata ongezeko la uhaulishaji wa teknolojia kati ya Watafiti na Jamii na kuwajengea uwezo waandishi wa habari ili waweze kuandika taarifa za Sayansi,Teknolojia na Ubunifu kama ilivyo katika maeneo mengine ikiwemo siasa na michezo”amesema Leonard




Discussion about this post