NA MWANDISHI WETU,DODOMA
MAKAMU wa Rais Dkt. Philip Mpango amewataka Wakuu wa Wilaya nchini kuzingatia utawala bora,kanuni na sheria ikiwemo kudhibiti uvujaji wa siri za serikali kwa kujiepusha na matumizi yasiofaa ya mitandao ya kijamii na barua pepe binafsi katika kutuma nyaraka za serikali.
Mbali na hilo lakini pia amewataka kuzingatia utaratibu katika matumizi ya walinzi binafsi na waandishi wa habari katika ofisi za umma pamoja na utatuzi wa migogoro katika maeneo yao.
Dkt.Mpango ameyasema hayo Machi 13, 2023 wakati akifungua Mafunzo ya Uongozi kwa Wakuu wa Wilaya yanayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Jiji la Dodoma uliopo Mtumba.
Amesema ni vema viongozi hao kuzingatia maadili ikiwemo kwa kujiepusha na matumizi yasiofaa ya mitandao ya kijamii na barua pepe binafsi katika kutuma nyaraka za serikali.
Amesema ni muhimu kwa viongozi hao kuwa wepesi na wabunifu katika kutatua migogoro hususani migogoro ya ardhi na mipaka, migogoro baina ya wakulima na wafugaji na baina ya wafugaji au wakulima na hifadhi na kuhakikisha hakuna migogoro mipya inayoibuka katika maeneo yao.
Ameongeza kuwa viongozi hao wana wajibu wa kudhibiti uhasama ndani ya jamii au na vyombo vya dola, mauaji na kuwa walinzi wa haki za watu wote hususani wanawake na watoto.
Hata hivyo Dkt.Mpango amewataka kusimamia miradi inayotekelezwa katika maeneo yao kwa kuhakikisha inakamilika kwa wakati na viwango vilivyokusudiwa na kuongeza jitihada katika ukusanyaji wa mapato ya ndani ya Halmashauri, kudhibiti matumizi yasiyo na tija pamoja na kuziba mianya yote inayosababisha fedha nyingi za Serikali kupotea na kuhakikisha malipo mbalimbali katika maeneo yao yanafanyika kielektroniki na fedha zinapelekwa benki kwa wakati.
Aidha amefafanua kuwa viongozi hao wanatakiwa kuwa walinzi maadili, mila , desturi na utamaduni wa mtanzania kwa kutofumbia macho mmomonyoko wa maadili wa aina yeyote utakaojitokeza katika maeneo wanayosimamia.
“Mjiepusha na rushwa, ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka pamoja na kutenda haki kwa wananchi na watumishi walio chini yao kuwahudumia wananchi kwa staha, kusikiliza kero na kuzitafutia ufumbuzi kwa wakati na kuwa makini wakati wote mnapozungumza na Umma kwa kuhakikisha mnatumia lugha fasaha na nzuri.
“Ni lazima pia kuimarisha utunzaji na uhifadhi wa mazingira kwa kutoa hamasa kwa wananchi hususani vijana ili wawe mstari wa mbele katika shughuli za uhifadhi ikiwemo kupanda miti na kusimamia mipango miji katika maeneo yao.”amesema Dkt.Mpango
Dkt Mpango ameongeza kuwa pamoja na masuala mengine lakini pia wasimamia suala la uhifadhi wa vyanzo vya maji na matumizi ya nishati mbadala ili kupunguza utegemezi mkubwa wa kuni na mkaa.
Kwa Upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaan (OR-TAMISEMI) Angellah Kairuki amesema Wizara hiyo imelenga kuongeza jitihada katika usimamizi wa miradi ya maendeleo, kuongeza jitihada katika ukusanyaji wa mapato na udhibiti wa matumizi, kuweka mkazo katika uwezeshaji wa wananchi kiuchumi, uendelezaji miji pamoja na kuhamasisha maendeleo vijijini.
Aidha amewataka Wakuu wa Wilaya kuhakikisha wanawahudumia vema wawekezaji na wenye nia ya kuwekeza hapa nchini kwa kuwa wafuatiliaji na kuondoa vikwazo kwenye masuala ya uwekezaji katika maeneo wanayosimamia.
Naye Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Jenista Mhagama amewaasa Wakuu wa Wilaya kuhakikisha huduma bora zinawafikia wananchi, kutenda haki kwa watumishi wote na kuwa na mshikamano ikiwemo kusimamia medani za siasa na utawala bora na kuwachukulia hatua watumishi wote wanaoenda kinyume na kanuni, sheria na miongozo ya utumishi wa umma.
Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Daniel Chongolo amesema ni muhimu kwa viongozi hao kusimamia kikamilifu suala la migogoro ya ardhi,wakulima na wafugaji ambayo inasababishwa na viongozi katika maeneo husika kutotimiza wajibu wao kikamilifu.




Discussion about this post