NA MWANDISHI WETU
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango ametoa wito kwa Jeshi la Polisi nchini kujitathmini mara kwa mara ili kuwa tayari kukabiliana na changamoto za nyakati hizi za mabadiliko makubwa kiteknolojia na kiuchumi.
Amesema Jeshi la Polisi linatakiwa kuwa kioo cha jamii katika usimamizi wa sheria hivyo ni vema kusimamia maadili mema, nidhamu kazini na uwajibikaji kwa wananchi.
Makamu wa Rais ameyasema hayo Aprili 28, 2023 wakati wa ufunguzi wa Mradi wa kituo cha Polisi Daraja “A” Gezaulole – Kigamboni mkoani Dar es salaam uliogharimu kiasi cha Tsh. Milioni 899.
Amesema ni muhimu kwa Jeshi la Polisi kujidhatiti vizuri katika eneo la upelelezi kwa kuwajengea uwezo vijana wake kupitia mafunzo zaidi katika vyuo mahiri kwenye masuala ya upelelezi hasa wa kesi za jinai ili kukabiliana na mbinu za kisasa za mitandao ya uhalifu nchini na hata Kimataifa.
Amebainisha kuwa hali hiyo itaondoa malalamiko ya wananchi kuhusu upelelezi wa kesi kuchelewa pamoja na wananchi kubambikiziwa kesi.
Ameongeza ni vyema pia Jeshi la Polisi likaangalia uwezekano wa kutumia TEHAMA na kuweka adhabu kali kwa wanaosababisha ajali pamoja na kuacha kupokea rushwa kutoka kwa madereva na kufumbia macho makosa ambayo hugharimu maisha ya watu wengi.
Aidha amefafanua kuwa bado taifa linakabiliwa na changamoto ya ajali ambazo zinasababishwa na madereva kutozingatia sheria za usalama barabarani, ulevi, ubovu wa magari pamoja na wengi wao kutokuwa na sifa za udereva.
Dkt Mpango amewaasa polisi kuwahudumia wananchi kwa staha, kusikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi kwa wakati pamoja na kuepukana na lugha za matusi, kejeli na dharau na kuongeza jitihada katika kukabiliana na ajali za barabarani hapa nchini ikiwemo kuimarishwa mahusiano baina ya Jeshi la Polisi na Wananchi ili kudhibiti uhalifu kwa urahisi.
“Uhusiano mzuri kati ya Jeshi la Polisi na raia utawawezesha wananchi kushirikiana na Polisi kudhibiti uhalifu na pia kuboresha ulinzi shirikishi hivyo ni muhimu kwa Jeshi hilo kuandaa mazingira salama ambayo yatawafanya wananchi kuwa na imani kwamba watasikilizwa, hawatadhalilishwa au kuchukuliwa kama wahalifu”amesema Dkt.Mpango

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi Mhandisi Hamad Masauni amesema Jeshi la Polisi halitashindwa kuthibiti uhalifu wowote ikiwemo uvunjifu wa maadili unaojitokeza hivi sasa.
Mhandisi Masauni amefafanua kuwa uzinduzi wa Vituo hivyo ni katika kuadhimisha miaka 59 ya Muungano ambao una lengo la kuimarisha udugu na usalama na hivyo kuwafanya wananchi kufanya shughuli za kiuchumi kwa amani na utulivu.
Awali akitoa taarifa za ujenzi wa kituo hicho Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillius Wambura amesema jeshi hilo limeendelea kuboreshwa ikiwa ni mkakati wa serikali wa kuimarisha na kuboresha miundombinu ya jeshi kwa kuzingatia mabadiliko ya sayansi na teknolojia kwa lengo la kuhakikisha haki za binadamu na utawala bora unadumishwa.
IGP Wambura ameongeza kuwa Jeshi la Polisi litaendelea kutunza rasilimali zilizopo ikiwemo miundombinu ya zamani na inayojengwa kwa sasa kwa mustakbali wa usalama wa nchi.
Amebainisha kuwa Jeshi hilo litaendelea kutekeleza majukumu yake kwa nidhamu, haki, weledi na uadilifu na litahakikisha linasimamia vema mafanikio ya Muungano kwa kulinda amani na utulivu uliopo.




Discussion about this post