NA GOODLUCK HONGO
SERIKALI kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imesema itaendelea kushirikiana na vyombo vya habari nchini katika kutoa elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa uhifadhi na utunzaji wa mazingira ikiwemo wa uhifadhi wa Tabaka la Ozoni.
Hayo yamesemwa Septemba 16,2023 jijini Dar es Salaam na Kaimu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais, Abdallah Mitawi wakati akifungua warsha ya mafunzo kwa waandishi wa vyombo vya mbalimbali vya habari kuhusu udhibiti wa uingizaji wa kemikali zinazodhibitiwa chini ya Itifaki ya Montreal iliyofanyika Septemba 16, 2023 jijini Dar es Salaam.
Mitawi amesema Tanzania kama nchi nyingine Duniani imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kukabiliana athari za matumizi vifaa vya kemikali vyenye ukomo wa matumizi kwa kuimarisha mifumo ya udhibiti wa kemikali hizo ambazo ambazo zina madhara mbalimbali katika jamii ikiwemo magonjwa, ongezeko la joto duniani na mabadiliko ya tabianchi.
“Tutaendelea kushirikiana na vyombo vya habari katika kuhakikisha elimu ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira inaifikia jamii.
“Tunatambua mchango mkubwa wa Chama cha Waandishi wa Habari za Mazingira (JET) kwani tangu kuanzishwa kwake mwaka 1991 imekuwa mstari wa mbele kuhamasisha jamii kutunza na kuhifadhi mazingira” amesema Mitawi.
Akifafanua zaidi Mitawi amesema ni takribani miaka 35 sasa tangu Jumuiya ya Kimataifa ilipoamua kuchukua hatua mahsusi za kunusuru tabaka la ozoni katika kulinda afya ya binadamu na mazingira ambapo mwaka 1987 ilipitishwa Itifaki ya Montreal kuhusu udhibiti wa kemikali zinazomong’onyoa tabaka hilo.
“Lengo kuu la Itifaki hii ni kupunguza uzalishaji na matumizi ya kemikali zinazomong’onyoa tabaka la Ozoni….Nafasi ya vyombo vya habari ni kubwa katika kuelimisha jamii kuhusu athari ya matumizi ya kemikali hizi ambapo zimeleta athari mbalimbali ikiwemo mabadiliko ya tabianchi” amesema Mitawi.
Amesema katika jitihada za kuhifadhi tabaka la ozoni, Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais imeandaa na kutekeleza programu na shughuli mbalimbali ikiwemo kuendelea kuhimiza jamii kupunguza shughuli za kibinadamu ambazo zinasababisha mabadiliko ya tabianchi pamoja na kutoa mafunzo kwa Maafisa Forodha na Wasimamizi wa Sheria maeneo ya mipakani.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Mazingira, Ofisi ya Makamu wa Rais, Bi. Kemilembe Mutasa amesema juhudi mbalimbali zimeendelea kufanywa na Serikali katika Tabaka la Ozoni ikiwemo amesema katika kuelekea Siku ya Tabaka la Hifadhi ya Ozoni kutoa mafunzo kwa mafunzo mchundo na maafisa wa forodha na wasimamizi wa sheria katika maeneo ya mipakani.
“Tanzania sio mzalishaji wa kemikali hizi,tumekuwa tukipokea kutoka nchi za nje..,tumeandaa kanuni, sera, sheria na miongozo mbalimbali katika kuelimisha jamii na pia Tumekuwa na mfululizo wa mafunzo haya kwa makundi mbalimbali ili kudhibiti kemikali hizi” amesema Kemilembe.
Naye Mtaalamu wa Kemikali kutoka Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Anania Kapatala amesema kemikali ikitumika vibaya huleta madhara makubwa na si kwa binadamu pekee bali hata mazingira.
“Sisi hushughulika na utoaji wa vibali vya kuingiza kemikali nchini na kwa sasa kemikali inayoongoza kuingizwa ni Amonium Nitrate na Sulphur ambapo nyingi hutumika katika migodi kwa ajili ya kulisulia miamba na nyingine kupelekwa nje ya nchi lakini sulphur ikimwagika haina madhara lakini ikipata maji huwa na madhara makubwa na hubakia muda mrefu katik ardhi”amesema Kapalaka
wanasheria kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais Mugisha Kyameni amesema makosa yote ya mazingira ni ya jinai na mtu akipatikana na hatia badi hufungwa kuanzia miaka mitatu,saba na faini kiasi cha Sh.Milioni 50 au vyote kwa pamoja.
Septemba 16, kila mwaka, Tanzania huungana na Jumuiya ya Kimataifa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la Ozoni ambapo Kauli mbiu ya Siku ya Kimataifa ya Hifadhi ya Tabaka la Ozoni mwaka 2023 ni “Hifadhi ya tabaka la ozoni na kupunguza athari za mabadiliko ya tabianchi”
MWISHO




Discussion about this post