MAWAZIRI wa Mambo ya Nchi za Nje wa Burkina Faso, Mali, na Niger wameidhinisha mipango ya kuunda shirikisho linalounganisha mataifa matatu yao ya Afrika Magharibi, ambayo kwa sasa yanatawaliwa na wanajeshi wao, kwa lengo la kukabiliana na changamoto za pamoja.
Uamuzi huo ulitangazwa katika taarifa ya pamoja iliyochapishwa kwenye X (zamani Twitter) siku ya Jumapili, kufuatia mkutano wa siku mbili katika Mji Mkuu wa Mali, Bamako, unaoangazia mipango ya kuendeleza Muungano mpya wa Nchi za Sahel (AES).
Watawala wa kijeshi wa makoloni matatu ya zamani ya Ufaransa walitia saini mkataba wa AES mwezi Septemba, wakikubali kusaidiana katika tukio la uchokozi wa nje au vitisho vya ndani kwa uhuru wao.
Mataifa hayo hapo awali yalikuwa wanachama wa makubaliano ya G5 Sahel yanayoungwa mkono na Paris, pamoja na Chad na Mauritania.
Makubaliano ya G5 tangu wakati huo yamesambaratika, kufuatia msururu wa mapinduzi ya kijeshi katika eneo hilo.
Muungano huo unaonekana kuwa na faida kwa nchi hizo ambapo Jeshi la Mali lilifanikiwa kuuteka na kuuthibiti kikamilifu mji wa Kidal uliokuwa ukikaliwa na waasi wa Tuareg kwa miaka 11 iliyopita
Mawaziri hao walifanya mkutano wao wa kwanza kutoka Alhamisi hadi Ijumaa na kukubaliana juu ya “hatua zinazofaa,” ikiwa ni pamoja na itifaki za kutekeleza mkataba wa AES.
“Mawaziri walipendekeza kuhimiza ushiriki wa wawakilishi waliochaguliwa, wanawake, vijana na mashirika ya kiraia katika mipango ya AES,” kulingana na taarifa ya pamoja.
Aidha walisisitiza umuhimu wa diplomasia na ulinzi katika kupanua ushirikiano wao wa kisiasa na kiuchumi.
Hapo awali, mawaziri wa fedha wa nchi hizo walipendekeza kuanzisha hazina ya kuleta utulivu na benki ya uwekezaji kwa AES, pamoja na “kamati iliyopewa jukumu la kuendeleza mijadala kuhusu masuala ya kiuchumi na muungano wa fedha.”
Waziri wa Mambo ya Nje wa Mali, Abdoulaye Diop, ambaye alimkaribisha mwenzake wa Burkinafaso Olivia Rouamba na Bakary Yaou Sangare wa Niger, walisema mapendekezo hayo yatawasilishwa kwa watawala wa kijeshi, ambao wamepangwa kukutana mjini Bamako katika tarehe ambayo haijatajwa.
Mwezi uliopita, kiongozi wa mapinduzi ya Niger Jenerali Abdourahamane Tchiani alisafiri hadi Mali na Burkina Faso, ikiwa ni safari zake za kwanza nje ya nchi tangu kuondolewa madarakani kwa Rais wa Niger Mohammed Bazoum Julai.
Jenerali Tchiani aliwashukuru viongozi wenzake wa Bamako na Ouagadougou kwa msaada waliotoa kwa Niamey, ambao alisema uliiwezesha Niger kustahimili vitisho kutoka kwa Umoja wa Afrika Magharibi wa ECOWAS.
ECOWAS muungano wa mataifa 15 umetishia kupeleka vikosi vya kijeshi dhidi ya watawala wa kijeshi wa Niger na umezuia akaunti za nchi hiyo katika benki kuu za kikanda ili kukabiliana na kupinduliwa kwa Rais Bazoum.




Discussion about this post