NA MWANDISHI MAALUM ZANZIBAR
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango amesema tafiti zinapaswa kufanyika kwa kina ili kubaini visababishi zaidi vya magonjwa ya moyo.
Amesema tafiti hizo zitasaidia kupata taarifa zaidi juu ya taratibu za kijamii na tabia za kiutamaduni katika mambo mbalimbali yaliyozoeleka kufanyika barani Afrika.
Mbali na hilo lakini pia jitihada inahitajika katika kutoa elimu ya magonjwa yasioambukiza pamoja na kuzingatia mtindo bora wa maisha, mazoezi na kufanya vipimo vya afya mara kwa mara ili kukabiliana na maradhi mbalimbali ikiwemo magonjwa ya moyo.
Dkt.Mpango ameyasema hayo Februari 9,2024 Unguja Zanzibar wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo uliyoandaliwa na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete na kuwatanisha Madaktari Bingwa, wataalam na wadau wa afya, wauguzi na watunga sera kutoka mataifa zaidi ya 40 duniani kwa lengo la kujadiliana na kubadilishana uzoefu katika masuala mbalimbali yanayohusu magonjwa ya moyo duniani .
Amesema katika kukabiliana na ugonjwa wa moyo ni muhimu wananchi kufuata njia za kujikinga zaidi ikiwemo kuacha ulevi uliyopindukia, uvutaji sigara, tabia bwete pamoja na uzito uliyopindukia.

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Philip Mpango akimkabidhi tuzo Muuguzi Kiongozi wa Kwanza wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Salome Kassanga wakati wa Ufunguzi wa Mkutano wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo unaofanyika Unguja, Zanzibar Februari 9,2024. (Picha na Ofisi ya Makamu wa Rais)
Amefafanuwa kuwa Tanzania imechukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya moyo kama vile kuimarisha Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, kufanya tafiti za afya za kimkakati ili kupata suluhu ya changamoto mbalimbali za kiafya zinazowakabili wananchi pamoja na kutoa elimu ya magonjwa yasiyoambukiza na magonjwa adimu.
”Taasisi ya Moyo ya jakaya Kikwete imeendelea kuimarika ambapo kwa sasa inafanya upasuaji kwa wagonjwa wa moyo 800 kwa mwaka ikiwemo upausaji wa kufungua kifua (upasuaji mkubwa) ukilinganisha na wagonjwa 200 wakati ikianzishwa.
”Zaidi ya wagonjwa laki mbili hutibiwa kwa mwaka huku zaidi ya 2400 wakitoa mataifa mengine na serikali imeweza kuokoa zaidi ya bilioni 63 kila mwaka za matibabu ya wagonjwa wa moyo kutokana na kuimarishwa kwa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete” amesema Dkt.Mpango.

Makamu wa Rais ameeleza kuwa serikali itaongeza uwekezaji katika huduma za magonjwa ya moyo na kuandaa mipango ya awali, ubunifu, tafiti , mafunzo, ushirikiano, udhibiti na utoaji tiba wa magonjwa ya moyo nchini.




Discussion about this post