NA MWANDISHI WETU,DODOMA
WATU 15 wakiwemo watoto 12 wamefariki dunia kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini huku Jeshi la Polisi likitoa tahadhari kwa wananchi kuchukua hatua za kujilinda.
Akizungumzia vifo hivyo kupitia taarifa iliyotolewa Aprili 8,2024 jijini Dodoma,Msemaji wa Jeshi la Polisi Naibu Kamishna wa Polisi DCP David Misime amesema kuanzia Aprili mosi hadi Aprili 7,2024 watu 15 wamefariki dunia kutokana na kusombwa na maji ya mvua zinazoendelea kunyesha huku wengine wakifariki kwa kuogelea na kutumbukia katika mashimo au madimbwi yaliyojaa maji.
‘’Miongoni mwa watu hao 15,watoto ni 12 na watu wazima ni watatu,matukio hayo yametokea katika wilaya mbalimbali nchini,mfano Wilaya ya Kalambo Mkoa wa Rukwa mwanaume mmoja mwenye umri wa miaka 18 alisombwa na maji yaliyokuwa yakitokea milimani wakati alipojaribu kuvuka daraja Aprili 1,2024
‘’Tarehe hiyo hiyo katika Wilaya ya Kilwa Mkoa wa Lindi,watoto wawili wote wakiwa na umri wa miaka 12 wakufa maji baada ya kusombwa na maji ya mvua,Aprili 2,2024 mwanaume mmoja wa miaka 28 katika Wilaya ya Ludewa Mkoa wa Njombe alikufa baada ya kufukiwa na udongo ulioporomoka kutokana na mvua kubwa zilizokuwa zinanyesha,Aprili 3,2024 huko wilayani Muheza Mkoa wa Tanga mtoto wa miaka nane alikufa maji wakati akiogelea,mkoani Pwani Aprili 3,2024 Wilaya ya Mkuranga mtoto mmoja wa miaka 10 alifariki dunia wakati akiogelea Mto Mzinga”amesema Misime
Kamanda Misime amebainisha kuwa wilayani Kibaha Mkoa wa Pwani mtoto wa miaka 12 alikufa maji yaliyokuwa yamejaa katika bonde la mpunga ambapo Aprili 5,2024 mwanamke mwenye umri wa miaka 55 alikufa maji mkoani Manyara baada ya kutumbukia kwenye shimo lenye maji.
‘’Aprili 7,2024 huko katika Wilaya ya Kyela Mkoa wa Mbeya watoto watano wenye umri kati ya miaka mitano na sita walifariki dunia baada ya kuzama kwenye dimbwi lililojaa maji ya mvua wakiwa wanaogelea,pia tarehe hiyo hiyo huko mkoani Geita watoto wawili wenye umri wa miaka tisa na 14 walifariki dunia baada ya kusombwa na maji ya mvua yaliyokuwa yanatiriria kutoka milimani wakitoka kuokota kuni
’Jeshi la Polisi kutokana na mtiririko wa matukio haya kwa mwezi huu Aprili na katika kipindi kifupi na uzoefu wa matukio mengine kama hayo ya siku za nyuma ,linaendelea kutoa wito na tahadhari kwa watu wote hususani wazazi na walezi kuwalinda watoto kwa karibu sana na kuwapa maelekezo sahihi kutokana mvua hizi zinazoendelea kunyesha
‘’Pia viongozi wa Serikali za Mitaa,Viongozi wa Dini na Walimu mashuleni tuendelee kuwaelemisha watoto wetu kujihadhari na maji yaliyotuama au yanayotembea na wala wasishindane na maji ya mvua yanayotiririka kwani ni hatari kwa maisha yao”amesema Misime
‘Misime ameongeza kuwa kila mmoja kwa nafasi yake akemee anapoona watoto wakicheza,wakipita au kuogelea katika maeneo hatarishi na sehemu ambazo zinastahili kuwekwa alama za tahadhari ziwekwe au kufunikwana kutolea mfano mashimo yaliyochimbwa kwa ajili ya visima vya maji majumbani na sehemu zingine.




Discussion about this post