NA MWANDISHI WETU
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan amesema Serikali iko pamoja na walimu na wanajua kazi kubwa wanayoifanya nchini.
Kauli ya Rais Samia imekuja wakati ambapo Serikali yake imeamua kuwapandisha madaraja walimu wote walioonekana kuwa na sifa za kupanda madaraja yao kihalali lakini walishindwa kupandishwa katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Tano iliyoongozwa na Hayati Rais Dkt.John Pombe Magufuli
Kupandishwa kwa madaraja ya walimu waliosotea miaka mitano iliyopita na wengine kufaidika kwa kupandishwa madaraja mawili ya lile waliopunjwa na muda wa sasa wa kupanda madaraja hayo ni ishara tosha kuwa Rais Dkt.Samia anatambua mchango mkubwa wa walimu na kuwathamini.
Akizungumza wakati wa ziara yake mkoani Rukwa Julai 16,2024 wakati alipotembelea Chuo cha Ualimu Sumbawanga na kuzindua majengo mapya ya chuo hicho Rais Dkt.Samia amesema analishukuru sana Kanisa kwa miaka yote kuwaruhusu kutumia majengo yao kutengeneza walimu.
Amesema maeneo yote wanayotumia ni lazima yatunzwe na kwamba chuo hicho kizalishe walimu na walimu na Serikali iko pamoja nao.
‘’Nataka niwaambie Serikali iko pamoja na nyie na tunajua kazi kubwa na ya thamani mnayoifanya,sisi tunajua lakini kubwa Mungu anajua mnachokifanya.
‘’Amani,utulivu na usalama tulionao ni kwa sababu walimu mnatengeneza watu wazuri kwa mimi niwaombe chapeni kazi ndugu zangu’’amesema Rais Dkt.Samia
Wakati huo huo akizungumza wakati alipotembelea Shule ya Sekondari ya Wasichana Rukwa Julai 17,2024 kuangalia uwekezaji uliofanyika na kama fedha zilizopelekwa na Serikali ikiwa zimetumika vizuri,Rais Dkt.Samia amebainisha kuwa faraja kubwa ni kwamba tayari wanafunzi wameshaanza kusoma.
Amesema hizo ni shule maalum ambazo zinajengwa moja kwa kila mkoa hivyo ni muhimu wanafunzi wakasoma kwa bidii na changamaoto walizonazo wanajitahidi kuziondoa ili wapate wasaa mzuri wa kusoma
‘’Tumeanzisha mfumo rasmi ndani ya Serikali,Scholarship rasmi kwa wanaofaulu vyema masomo ya sayansi kwa wanaume na wanawake’’amesema Rais Dkt.Samia
‘Daraja la mserereko’
Awali Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMII) Dkt Charles Msonde alitembelea baadhi ya Halmashauri na kukutana na walimu ambapo alisisitiza nia ya Serikali ya kuhakikisha kuwa hakuna mwalimu atakayeachwa hasa wale walioshindwa kupandishwa madaraja yao kihalali miaka iliyopita
Dkt.Msonde aliwahakikishia walimu hao kuwa hata kama mwalimu alipunjwa daraja lake lakini pia mwaka huu anasifa ya kupanda daraja basi atapata yote mawili.
Moja ya Manispaa ambazo Dkt.Msonde alikutana na Walimu ni Manispaa ya Temeke mkoani Dar es Salaam.
Uchunguzi uliofanywa na Bajeti Communication umegundua kuwa tayari walimu wengi wameshapata madaraja yao waliopunjwa maarufu kama mserereko
Hata hivyo jina la ‘mserereko’ linatokana na walimu hao kukata tamaa ya kulipata daraja hilo kwa kuwa muda wake wa kupandishwa ulishapita miaka mingi nyuma hivyo kulipata imekuwa kama ndoto.



Discussion about this post