NA MWANDISHI WETU,MWANZA
WATANZANIA wametakiwa kuwaenzi Mashujaa waliopoteza Maisha yao Wakiutetea, Kuupigania na Kulinda Uhuru wa Tanzania kwa kulinda amani iliyopo ambayo matunda yake yanamfaidisha kila mmoja.
Mbali na hilo lakini pia wametakiwa kuienzi misingi imara ya kizalendo ya amani na upendo iliyojengwa na waasisi wa Taifa ikiongozwa na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume.
Wito huo umetolewa Julai 25,2024 na Katibu Tawala wa Wilaya ya Magu mkoani Mwanza Jubilate win Lawuo wakati wa kuadhimisha siku ya mashujaa inayoadhimishwa kila ifikapo Julai 25 ya kila mwaka.
Lawuo amesema ni muhimu kwa Wananchi wa Magu na maeneo mengine ya Tanzania kuendelea kuwaenzi Mashujaa kwa kuwa Wazalendo na kulinda amani ya nchi kwani ndio Msingi wa Maendeleo ya Taifa.
Amesema watanzania wote wanatakiwa kuienzi misingi imara ya kizalendo ya amani na upendo iliyojengwa na waasisi wa Taifa ikiongozwa na Baba wa Taifa Hayati Mwl. Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume, misingi ambayo matunda yake yanawafaidisha watanzania wote hivyo ni muhimu kujipanga ili kurithisha vizazi vijavyo.
“Tumekuja hapa kwa ajili ya kumbukumbu ya wazalendo wetu waliojitoa kipindi hicho katika kulipigania Taifa letu na matunda yake tunayaona hadi leo na vizazi vyetu vitakuja kufaidi matunda haya hivyo ni vema tujipange kurithisha vizazi vijavyo” amesema Lawuo.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Magu Mohamed Ramadhani amebainisha kuwa Magu inawakumbuka mashujaa kwa kujitoa kwao na kusababisha Taifa kupata ukombozi ambao hadi sasa watanzania wanaendelea kufaidi matunda yaliyotokana na kujitoa kwao.
‘’Funzo kwetu ni kuwa wazalendo kwa nchi yetu kama walivyokuwa Mashujaa wetu ambao walijitoa kwa hali na mali’’ameongeza Ramadhani
Hata hivyo Ramadhani amewakumbusha Wananchi kutunza mazingira ya Wilaya kwa ajili ya Afya ya Jamii huku akiwahimiza kufanya usafi kuwa sehemu ya maisha yao ya kila siku na sio kusubiri matukio maalumu.
Akizungumza kwa niaba ya viongozi wa Dini na Shekh Mkuu wa Wilaya ya Magu,Shekh wa Kata ya Isandula Majaliwa Rashid ambaye amesema viongozi wa dini wataendelea kuwakumbuka mashujaa kwa kuwaombea dua kwa mazuri waliyofanya na kusema kuwa wataendelea kuliombea Taifa liendelee kuwa na amani, upendo na mshikamano.
Wilaya ya Magu katika kuadhimisha siku hiyo pia iliambatana na shughuli mbalimbali kufanya usafi katika Hospitali ya Wilaya ya Magu na maeneo mengine ikiwemo dua na sala maalumu za kuwaombea Mashujaa waliopoteza maisha yao na walio hai na kuombea Amani .
Kila ifikiapo Julai 25 ya kila mwaka,Tanzania huadhimisha siku ya kuwakumbuka Mashujaa waliopoteza Maisha yao Wakiutetea, Kuupigania na Kulinda Uhuru wa Tanzania.




Discussion about this post