NA MWANDISHI WETU,MOROGORO
WANANCHI wa Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro wametakiwa kutumia Majiko Banifu yanayotolewa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika Maonesho ya Samia Kilimo Biashara Expo 2024, kwa kuwa yanatunza mazingira na rafiki kwa afya ya watumiaj.
Hayo yamebainishwa Oktoba 6, 2024 na Mkuu wa Wilaya ya Gairo mkoani Morogoro,Jabir Makame wakati akizungumza na wananchi mara baada ya kutembelea banda la REA yanapofanyika maonesho hayo kwa msimu wa tatu katika kijiji cha Leshata wilayani humo.
Makame ameeleza kuwa, majiko banifu ni rafiki na salama kwa afya ya watumiaji nchini na kuwasisitiza wananchi kuyatumia kwa kuwa yanauzwa na kupatikana kwa gharama nafuu.
Makame amesema wananchi hao wanakwenda kushuhudia mageuzi makubwa ya utunzaji wa mazingira kupitia Mkakati wa Matumizi ya Nishati Safi ya Kupikia ambao kinara wake ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Aidha ameeza kuwa Gairo inatekeleza kampeni ya ‘’URITHI WA KIJANI yenye lengo la kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi ambayo yana athari katika Sekta ya Kilimo na Mifugo.
Ametaja wadau wanaoshiriki kuwa ni pamoja na Mashirika ya Mazingira, Kampuni za Gesi, Kampuni zinazotengeneza mkaa mbadala, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira pamoja na Wizara ya Nishati.
Naye, Mhandisi wa REA Deusdedith Malulu ameongeza kuwa, majiko hayo yanatunza mazingira kwa kutumia kiasi kidogo cha mkaa na ufanisi wake ni mkubwa.
“Majiko haya hayaruhusu hewa ya mkaa ambayo ni hatari kwa watumiaji kutoka nje kwa aina ya muundo wake na hivyo kuwa rafiki kwa mazingira” amesema Mhandisi Maluku
Mhandisi Malulu ameongeza kuwa kupitia maonesho hayo wananchi wa wilaya hiyo wameanza kupatiwa majiko banifu na REA imeaza kutoa majiko 790 ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha ajenda ya matumizi ya nishati safi ya kupikia nchini.




Discussion about this post