NA GOODLUCK HONGO,LINDI
MAKUMI ya watu na raia wa kigeni kutoka nje ya nchi wamesababisha kukauka kwa Mti maarufu wa Mwalimu Julius Nyerere uliopo katika Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia- Rondo baada ya kuingia usiku wa manane na kisha kubandua magamba yake.
Msitu huo unaopatikana katika Halmashauri ya Mtama mkoani Lindi ni kati ya misitu 23 iliyopandishwa hadhi na kuwa Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia kutokana na kuwa na mimea na wanyama wasiopatikana katika eneo lingine duniani.
Mti huo ambao unaelezwa kuwa ikiwa utafanikiwa kupata gamba lake na kisha kuliloweka katika maji na baadaye kuoga maji hayo basi utafanikiwa katika mambo yako yote unayoyahitaji.

Licha ya maajabu ya Mti wa Mwalimu Nyerere kuwa katika eneo hilo la Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia lenye mimea na wanyama wasiopatikana sehemu nyingine yoyote duniani lakini pia kuna miti ya ajabu yenye mizizi zaidi ya urefu wa futi nane.
Msitu huo ambao unaolindwa na kuhifadhiwa na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) umendelea kuwa eneo maarufu kutokana na kuwa na miti ya asili ambayo haijapandwa na mtu yeyote wala mazingira yake kuhusishwa na binadamu kuyatengeneza.

Watafiti kutoka kona mbalimbali za dunia hufika katika msitu huo kufanya tafiti mbalimbali kutoka katika miti ya asili inayopatikana katika eneo hilo pekee duniani.
Makumi ya watu wakiwemo wenyeji wanaozunguka msitu huo hufika katika eneo hilo kwa ajili ya kuomba na kufanya matambiko ikiwemo kupata mvua,kuondoa mikosi na kufanikiwa kimaisha.
Bajeti Communication ilifika katika eneo hilo na kujionea Mti huo maarufu wa Mwalimu Nyeyere uliopo ndani ya msitu mnene uliosheheni miti mikubwa ikiwa na mizizi yenye urefu zaidi ya futi tatu kwenda juu.
Akizungumza hivi karibuni katika eneo la Rondo juu ya Msitu huo,Afisa Mhifadhi Mkuu na Mkuu wa Hifadhi ya Msitu wa Hifadhi ya Mazingira-Rondo John Olomi,amesema hifadhi hiyo ni mojawapo ya hifadhi 23 zilizopandishwa hadhi na kuwa Hifadhi ya Mazingira Asilia nchini Tanzania.
Amesema ndani ya msitu huo wa hifadhi ya mazingira asilia kuna mimea muhimu sana ambayo inapatikana katika eneo hilo pekee na ipo hatarini kutoweka wakiwemo wanyama ambao hawapatikanani duniani zaidi ndani ya msitu huo.
Amesema hifadhi hiyo imepewa nafasi hiyo kwa sababu za huduma nyingi za kiikolojia ikiwemo hali ya hewa na ni hifadhi ya lindimaji ambapo muonekano wake ni eneo lililoinuka kwa maana ya plateau

Akizungumzia kuhusu Mti wa Mwalimu Nyerere,Olomi amebainisha kuwa mwaka 1978 Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alifika katika hifadhi hiyo na kisha kuchukua gamba ambapo kwa mujibu wa Kabila Wamwela ambao ndio wenyeji wa eneo hilo wanaamini kwamba kitendo hicho kilikuwa na baraka nyingi sana hivyo jamii na watu mashuhuri mbalimbali hufika na kutembelea mti huo.
‘’Lengo ni kupata Baraka au kusema shida zao,au kuombam mafanikio mbalimbali kutokana na namna wanavyoona wao na wamekuwa wakitoa ushuhuda wa kufanikiwa kwako
’Mbali na hilo lakini imebainika katika hifadhi hii kuna mimea na wanyama wanaopatikana katika hifadhi hii ni wale ambao wanawezesha tafiti mbalimbali kufanyika na tunawaalika watafiti mbalimbali wanaopenda kufanya tafiti kuja ndani ya hifadhi yetu kwani bado tuna utajiri mkubwa wa mimea pamoja na wanyama ambao hawapatikani sehemu nyingine zaidi ya maeneo haya.
‘’Tunawaalika wananchi na wageni wetu kutoka maeneo mbalimbali kuja kwenye hifadhi yetu ya Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia-Rondo kwa ajili ya kufanya shughuli nyingi za kiutalii kwani bado msitu wetu una hifadhi kubwa ya mazingira asilia ya kufanya shughuli za kitalii”amesema Olomi

Naye Afisa Uhifadhi wa Msitu huo Ahazi Shayo ameeleza kuwa hifadhi inazungukwa na vijiji sita ambavyo kabila kuu katika eneo hilo ni Wamwela.
Amesema Mti huo ambao uko katikati ya Msitu mnene na lichen ya wao kuulinda kwa nguvu zote hasi usiku wa ,manane,wananchi wamekuwa wakitumia njia mbalimbali ili kubandua magamba yake na kuondokana nayo
Shayo amefafanuwa kuwa kuwa wakati waliwahi kuwakamata raia wa kigeni kutoka nchini Libya ambao walikuwa na mtu anayedaiwa kuwa ni mganga wa dawa za kienyeji kutokana nchini Msumbiji wakiwa katika eneo hili la hatari majira ya usiku.
‘’Walikuwa na mwenyeji wao na walipotuona walikimbia sasa hivyo ndivyo tunavyopambana kuulinda mti huo lakini wananchi wanafika usiku bila kuogopa wanyama na kubandua magamba na wengine kuomba hapa hapa na kuweka hela katika mti huu’’amefafanuwa Shayo
Bajeti Communication imeshuhudia mti huo ukiwa umekauka baada ya kubanduliwa magamba yote katika eneo lake la chini na kuyaacha yaliyo juu zaidi hali iliyoonekana kusababisha kukauka kwa mti huo
Hata hivyo baadhi ya wanakijiji wanaozunguka msitu huo wamesema Mwalimu Nyerer alipofika katika eneo hilo alitaka kutafutiwa mti huo aina ya Mkufya ili kupata gamba lake.
Wamesema walipomuuliza sababu ya kuchukua gamba la mti huo Mwalimu Nyerere aliwajibu kuwa mama yake amemtuma miti 100 ya kutengeneza dawa na mti uliokuwa umebakia ndio huo wa Mkufya ambao aliupa Londo katika Msitu huo wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Rondo.






Discussion about this post