NA GOODLUCK HONGO
KAMISHNA Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) Aretas Lyimo amesema wataendelea kukamata’ mapapa’ wa biashara ya dawa za kulevya nchini na kwamba Serikali hairogwi hata siku moja.
Hata hivyo Kamishna Jenerali Lyimo amewaonya wamiliki wa nyumba kuwa makini wanapopangisha nyumba zao kwani nyumba inayotumika kwa shughuli za dawa za kulevya inaweza kutaifishwa .
Kauli ya Kamishna Jenerali Lyimo imekuja baada ya kuwakamata ‘mapapa’wengine wa biashara hiyo waliotumia magari na boti huku baadhi yao wakiaminishwa na waganga wa tiba asili kuwa hawezi kukamatwa na hutumia nyumba walizopanga kuhifadhi na kufanyia biashara hiyo.
.DCEA ambayo imekamata tani 2.2 za dawa za kulevya katika mikoa ya Tanga na Dar es Salaam kwa mwezi Novemba pekee imeapa kuendelea na operesheni zake hadi biashara hiyo itakapotokomezwa kabisa.
Athari za dawa za kulevya zinapoingia mitaani haziathiri tu waliokwishaanza kutumia bali pia ‘mapapa’ wa biashara hiyo huwalenga watu wengine ambao hawajaanza kutumia ili kutanua masoko yao.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Novemba 25,2024, Kamishna Lyimo amebainisha kuwa baadhi ya watuhumiwa wanaowakamata huwaeleza kuwa huwa wanaaminishwa na waganga wa kienyeji kuwa hawawezi kukamatwa wanapofanya biashara hiyo.
‘’Serikali hairogeki hata siku moja,na sasa tunafanya utafiti lakini baadaye tutawakamata pia waganga kwani tunapiga mijini na vijijini kote tunafanya operesheni na itafika wakati dawa za kulevya nchini hazitapatikana na wafanyabishara wataishia gerezani’’amesema Kamshna Jenerali Lyimo
Akizungumzia operesheni waliyofanya mikoa wa Tanga na Dar es Salaam,Kamishna Jenerali Lyimo amebainisha kuwa DCEA kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama imekamata jumla ya kilogramu 2207.56 za dawa za kulevya na dawa tiba zenye asili ya kulevya katika mikoa hiyo ambapo watuhumiwa saba wanashikiliwa kwa tuhuma hizo.
Amesema kati ya dawa zilizokamatwa ni pamoja na Bangi aina ya Skanka kilogramu 1,500.6,Methamphetamine kilogramu 687.76,Heroin kilogramu 19.20 na chupa 10 za dawa tiba zenye asili ya kulevya aina ya Fentanyl.
‘’Novemba 14,2024 jijini Dar es Salaam,katika Wilaya ya Kigamboni ,Mtaa wa Nyangwale,watuhumiwa Mohamed Suleiman Bakarm na Sullesh Said Mhailoh wote wakazi wa Mabibo,Dar es Salaam walikamatwa wakiwa na kilogramu 1,350.4 za dawa za kulevya aina ya skanka,dawa hizo zilikuwa zimefichwa ndani ya nyumba aliyopanga mtuhumiwa Mohamed ambaye alitumia kama ghala la kuhifadhia dawa hizo.
‘’Aidha dawa nyingine zilipatikana ndani ya gari aina ya Nissan Juke yenye namba za usajili T534 EJC zikiwa tayari kwa kusambazwa’’ameeleza Kamishna Jenerali Lyimo
Hata hivyo ameongeza kuwa tarehe hiyo hiyo ,katika mtaa wa Pweza Sinza E Wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam mtuhumiwa Iddy Mohamed Iddy mkazi wa Chanika Buyuni alikamatwa akiwa na kilogramu 150.2 za skanka zilizofichwa katika maboksi ya sabuni.
‘’Baadhi ya dawa hizo zikiwa zimefichwa kwenye boksi lililotengenezwa kwa bati gumu na kupachikwa kwenye chassis ya gari aina ya Scania lenye namba za usajili wa Afrika Kusini LN87XJGP ambalo limekuwa likitumika kusafirisha bidhaa mbalimbali kutoka nje ya nchi.
‘’Novemba 17,2024 katika Jiji la Tanga watuhumiwa Ally Kassim Ally na Fahad Ally Kassim walikamatwa mtaa wa Mwakibila wakiwa na kilogramu 706.96 za dawa za kulevya aina ya heroin na methamphetamine na baadhi ya dawa hizo zilipatikana ndani ya gari aina ya Toyota Noah yenye namba za usajili T714 EGX huku nyingine zikibainika kufichwa kwenye nyumba aliyopanga mtuhumiwa. .
‘’Tarehe 19,Novemba 2024 katika Mtaa wa Kipata na Nyamwezi Kariakoo jijini Dar es Salaam watuhumiwa Michael Dona Mziwanda mkazi wa Tabata Segerea na Tumpale Bernad Mwasakila mkazi wa Temeke Mikoroshini walikamatwa wakiwa na chupa 10 za dawa tiba zenye asili ya kulevya aina ya Fentanyl wakiwa nazo katika duka’’ameongeza Kamishna Jenerali Lyimo
Mamlaka hiyo imewashukuru wananchi wanaotoa ushirikiano kwa kuwafichua watu wanaojihusisha na dawa za kulevya na wanawahimiza wote kuendelea kutoa taarifa pale wanapobaini matukio yanayohusiana na biashara haramu ya dawa za kulevya



Discussion about this post