NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha African Democratic Allience (ADA-TADEA) kimesema kina imani kubwa na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kutokana na maboresho makubwa yaliyofanyika hivyo kuufanya Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025 kuwa huru na wa haki.
ADA-TADEA ambacho kilianzishwa na Oscar Kambona 1991 kimebainisha kuwa vyama 18 kwa sasa vinaendelea na shughuli zao za kisiasa na kichama hivyo kuhidhirisha kuwa hali ya kisiasa iko shwari.
Akizungumza na Bajeti Communication Agosti 6,2025 jijini Dar es Salaam,Katibu Mkuu wa Chama hicho Salehe Msumari amebainisha kuwa INEC imejipanga kuhakikisha kuwa uchaguzi huu utakuwa huru na wa haki kwa kufanya maboresha mbalimbali ambayo wao kama wapinzani walikuwa wanayalalamikia sana.
Msumari ameongeza kuwa wanaishukuru Serikali kwa kusikikliza malalamiko ya wadau katika baadhi ya sheria katika Tume ambapo mengi ya msingi yamefanyiwa kazi huku ikiwashirikisha kila kitu.
Msumari ameyataja baadhi ya mambo waliyokuwa wakiyalalamikia kama vyama vya upinzani ni pamoja na kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi ambalo hilo limetekelezwa.
“Hakuna mgombea ambaye atapita bila kupingwa sasa hivi,hilo halipo,lazima mgombea apigiwe kura za ndio au hapana na kura za ndio ziwe nyingi ndio atapita lakini akipata za hapana nyingi basi Tume itaangalia.
“Mabadiliko mengine ni mfumo wa muundo wa Tume ambapo tulilalamika sana kuhusu Wakurugenzi wa Halmashauri kusimamia uchaguzi hivyo sasa hivi Tume wanawafanyakazi wao”amesema Msumari.
“Wenyewe wametuambia kabisa mtakapoona mtu atendi au anakwenda kinyume na maadili ambayo wao wamewaelekeza basi tuwape taarifa na wao watashughulika naye”amesema Msumari
Msumari amebainisha kuwa mbali na hayo lakini pia INEC imewakabidhi nyaraka mbalimbali zinazohusu uchaguzi ikiwemo orodha ya wapiga kura,ratiba,sheria pamoja na kuwahakikishia kuwa kampeni zifanyika kwa amani ikiwemo ulinzi kwa wagombea nafasi ya urais na katika mikutano ya hadhara.
“Wametueleza kuwa kama kuna dosari ndogondogo za mtu badala ya kuandika jina la chama kwa kirefu na akaandika kwa kifupi hilo halitakuwa tatizo.
“Sasa hivi wakala akiwa na kitambulisho cha kupigia Kura,Uraia na Leseni vinaweza kumtambulisha hata kama hana picha ambapo pia majina yote ya mawakala wanaosimamia kituo hicho yatabandikwa nje kila mtu ataona.
“Yale tuliokuwa tunayalalamikia mengi yamerekebishwa kwa asilimia 80 lakini mengine yanafanyika kutokana na utashi wa mtu binafsi na sio Tume kama Tume”amebainisha Msumari
Akizungumzia mikakati ya Chama chao,Msumari amebainisha kuwa ifikapo Agosti 10,2025 wagombea wote wa nafasi ya ubunge lazima fomu zao ziwe zimefika Makao Makuu ya Chama ambapo Agost 11,2025 watakaa Kikao cha Kamati Kuu kwa ajili ya kuwapitia wagombea hao na kuwapitisha.
“Fomu zote zitarudishwa INEC Agosti 27,2025 ambapo Agosti 28 kampeni zitaanza,lakini INEC imeruhusu wagombea wa nafasi ya urais kuwasilisha fomu zao Agosti 24,2025 ili wazihakiki kwanza na kama kuna makosa basi wataelezwa ili warekebishe kabla ya kuziwasilisha rasmi Agosti 27,2025”ameongeza Msumari
Hata hivyo Msumari ameongeza kuwa wametoa ofa kwa wagombea wanawake na watu wenye ulemavu kuchukua fomu bure kutokana na makundi hayo kutopewa kipaumbele na mazingira yao ya kiuchumi,
“Fomu ya kugombea nafasi ya Urais ni Sh.200,000,Ubunge Sh.30.000 na Udiwani ni Sh.20,000 lakini wanawake na wenye ulemavu ni bure ili kuwavutia kugombea nafasi hizo”ameeleza Msumari




Discussion about this post