NA MWANDISHI WETU
CHAMA Cha ACT Wazalendo kimesema kitafanya uchunguzi huru na wa kitaalam wa matukio yote ya utekaji, utesaji, upoteaji na mauaji ya raia ikiwemo kuchukua hatua dhidi ya wote wanaohusika ndani ya siku 100 baada ya kushika dola.
Hata hivyo chama hicho kimedhamiria kuhakikisha kuwa Tanzania inakuwa sehemu salama kwa wananchi kufanya shughuli zao, kuishi na kupiga hatua za maendeleo bila hofu, wasiwasi na mashaka.
Hayo yamebainika katika Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho ya 2025-2030 iliyozinduliwa Septemba 22,2025 jijini Dar es Salaam ikiwa itapata ridhaa ya kuchaguliwa na wananchi katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025 na kuunda Serikali itakayoundwa na chama hicho.
Hata hivyo ACT-Wazalendo imezindua Ilani yake wakati ambapo mgombea wake wa nafasi ya Urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Luhaga Mpina akienguliwa kugombea nafasi hiyo na Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) ambapo awali alikuwa amepitishwa na kukabidhiwa gari aina ya Land Cruiser kwa ajili ya kufanyia kampeni zake kabla ya kuwekewa pingamizi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali Johari Hamza.
Ilani hiyo imebainisha kuwa katika kuhakikisha Ulinzi na Usalama wa Raia na Serikali ya ACT Wazalendo itafanya uchunguzi huru na wa kitaalam wa matukio yote ya utekaji, utesaji, upoteaji na mauaji ya raia na kutoa ripoti ya kina kwa umma na kuchukua hatua dhidi ya wote wanaohusika ndani ya siku 100.
Mbali na hilo lakini pia itatoa msaada wa kisaikolojia, kijamii na kiuchumi kwa watu na jamii zilizoathiriwa na vitendo vya ukiukwaji haki.
“ACT-Wazalendo italiunda upya Jeshi la Polisi na kuliimarisha kitaaluma, kwa kulitoa kuwa chombo cha mabavu‘ (police force) na kulifanya kuwa chombo cha huduma (police service)
“Itakomesha vitendo vya utekaji, utesaji, uonevu, ubaguzi wa kiitikadi, unyanyasaji, uvunjifu wa haki za binadamu na mauaji ya raia na kuvunja magenge yote ya uhalifu na kuwachukulia hatua kali watu wote wanaohusika na vitendo hivyo.
“Itaipa uwezo wa kibajeti, kiweledi na kisheria Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora na Ofisi ya Uwakili wa Umma, ili kusimamia vyombo vya dola kulinda haki na usalama wa watu na mali zao kwa uhuru”imeeleza Ilani hiyo.
Ilani hiyo imefafanuwa kuwa itafanya mapitio ya Sheria ya Usalama wa Taifa na kuwaondolea mamlaka waliyopewa ya kukamata na kuwashikilia watu bila kuchukua hatua za sheria (arbitrary detention) na kufanya marekebisho ya sheria ya ugaidi na sheria nyingine kandamizi zinazotumika kiholela kwa ajili ya kupora haki za wananchi.
“ACT-Wazalendo itatunga sera ya mfumo wa Haki za Kijinai [Criminal Justice Policy] ili kuimarisha mifumo ya kitaasisi na kiuendeshaji wa taasisi za usimamizi wa jinai.
“Itaboresha mfumo wa upelelezi wa mashauri kwa kusimamia na kuweka ukomo wa muda wa upelelezi kwa makosa yote ili kupunguza mrundikano wa kesi.
“Itatunga sheria moja ya dhamana (Bail Act) kwa makosa yote ya jinai na kuweka utaratibu wa dhamana kwa makosa yote”imeongeza Ilani hiyo
Aidha chama hicho kupitia Ilani yake imeongeza kuwa itaimarisha utaratibu wa upatikanaji taarifa, uchunguzi na doria kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama ili kudhibiti matukio ya uhalifu na mauaji mijini na vijijini
Kwa upande wake Kiongozi wa chama hicho Doroth Semu amesema ACT Wazalendo inakuja na matumaini mapya na wanatambua kwamba Taifa linaweza kuongozwa kwa haki, uwazi, na misingi ya ushiriki wa wananchi kikamilifu.
“Tumedhamiria kujenga Taifa la Wote kwa Maslahi ya Wote, Taifa ambalo kila Mtanzania, popote alipo, anaweza kuishi kwa heshima, kupata huduma bora, kufanya kazi kwa uhuru na kunufaika na rasilimali za nchi yake.
“Ilani hii inabeba maono ya kuijenga Tanzania mpya – Taifa la Wote kwa Maslahi ya Wote.
“Taifa ambalo watoto wote wanapata elimu bora bila kulipishwa, wala kuchangishwa na kila mwananchi anapata huduma ya afya bila kuingia kwenye umasikini wakiwemo wakulima, wafugaji, wavuvi na wamachinga wanatambuliwa, kuheshimiwa na kuwezeshwa”amebainisha Semu


Discussion about this post