NA MWANDISHI WETU
SERIKALI ya Chama Cha African Democratic Alliance(ADA-TADEA) itapiga marufuku wanafunzi elimu ya juu (wanachuo) kupanga nyumba mitaani ikiwa itapata ridhaa ya kuchaguliwa na wananchi kuongoza nchi katika Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba 29,2025.
Hata hivyo ADA-TADEA imebainisha kuwa mabadiliko ya Elimu yatafuata mkondo wa Serikali ya awamu ya kwanza ambapo elimu kuanzia chekechea hadi Chuo Kikuu itakuwa bure.
Hayo yamebainika ndani ya Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025-2030 ya chama hicho iliyozinduliwa Septemba 14,2025 Mbagala mkoani Dar es Salaam muda mfupi baada ya kuzindua kampeni za urais,ubunge na udiwani ili kuwanadai wagombea wao nchi nzima.
Ilani hiyo imebainisha kuwa wanachuo wote watakuwa wanalipwa posho ya kujikimu kila mwezi, na utaratibu wa kupewa malazi na chakula bure utarejeshwa ili wasome kwa makini na bidii zaidi.
“Aidha, vyuo vyote ni lazima viwe na hosteli zao, itakuwa marufuku wanachuo kupanga ovyo mitaani kwa kuwa imeonesha kuathiri Masomo na Maadili yao.
“Chama cha African Democratic Alliance (ADA-TADEA) kitaweka mkazo maalum katika maktaba na elimu mtandao (libraries and eLearning) kwenye shule zote.
“Kutunga sheria maalum kuhakikisha taasisi zote za Serikali zinatumia mitandao wa Serikali kuhakikisha maeneo yote ya elimu yanatumia mtandao bila vikwazo”imeongeza Ilani hiyo
Mbali na hilo, ADA-TADEA itaanzisha kanzidata ya wahitimu wote kufahamu mwaka waliomaliza na utaalamu waliosomea ambapo ajira zitafuata umalizaji wao na aliyeanza kumaliza chuo ndiye atakayekuwa wa kwanza kupata ajira {First In First Out [FIFO]} na elimu itakuwa inaandaliwa kulingana na mabadiliko ya teknolojia na mwelekeo wa Dunia.
Serikali ya ADA=TADEA itaangalia upya viwango vya kuajiri na kusajili watumishi wa umma akiwemo Mwalimu wa Tanzania.
“Mtu akiajiriwa, Chama cha African Democratic Alliance (ADA-TADEA) kitahakikisha kinaboresha maslahi ya Waalimu wote.
“Walimu ambao wanapangiwa kwenye maeneo yenye changamoto nyingi watapewa posho maalum ikiwemo posho ya nyumba (accommodation allowance),
“Serikali itahakikisha nyumba za Walimu zinajengwa haraka kwenye maeneo ambayo ni vigumu kufikika na yenye mazingira magumu”imeongeza Ilani hiyo
Ilani hiyo imefafanuwa kuwa Ukaguzi wa Shule utaangaliwa upya na kuboreshwa ili kujua hali ya Waalimu na Wanafunzi ikoje na kama wanawajibika
“Tutahakikisha wazazi wanajihusisha na wanafunzi, ikiwemo kushiriki kwenye kamati za maendeleo ya shule na kamati zake ndogo, hii itasaidia kuleta utaalamu na weledi mbalimbali walionao wazazi.
“Hali hiyo itongea kiwango cha elimu kwa shule”imeleza Ilani hiyo
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Chama hicho Salehe Msumari ameelezea ilani yao kuwa ni bora kuliko za vyama vingine na kwamba ADA-TADEA kimekuwa na kuendeela kupanuka kutokana na hamu ya wananchi kujikomboa kutoka kwenye uchumi hodhi,utumwa wa fikra za ukoloni mambo leo na nguvu ya ubeberu
“Chama hiki kiliundwa kwa lengo la kuleta mabadiliko kawa amani ya kisiasa nchini Tanzania yaliyoongozwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Tanzania African National Union (TANU) na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa awamu ya kwanza Hayati Oscar Salathiel Kambona(1925-1997)”amesema Msumari



Discussion about this post