NA GOODLUCK HONGO
MDHIBITI na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Charles Kichere ameonya juu ya hatari ya kuwepo kwa mimea vamizi inayosambaa kwa kasi hasa katika maeneo ya hifadhi za Taifa na kuhatarisha mifumo ya ikolojia kwani baadhi yake ni sumu.
Mbali na baadhi kuwa sumu lakini pia huondoa mimea asilia na malisho na hailiwi na wanyamapori.
CAG Kichere amekuwa akitoa taarifa ya janga hilo kwa miaka mitano mfululizo lakini hatua zinazochukuliwa na Serikali zikionekana kuwa ndogo na kushauri litangazwe kama suala la kitaifa ili wadau wengine waweze kusaidia.
CAG Kichere katika ripoti yake kwa mwaka wa fedha 2024/25 ya Mashirika ya Umma ameeleza juu ya kusambaa na kuongezeka kwa kasi kwa mimea vamizi zaidi ya uwezo wa hifadhi kudhibiti.
Amesema amekuwa akiripoti juu ya kuenea kwa mimea vamizi na kupendekeza kwa Serikali kutangaza uvamizi huo kama suala la kitaifa na kuhusisha wadau wote katika kuondoa, kudhibiti, na kuzuia uwepo wake ndani ya Hifadhi ya Ngorongoro, Hifadhi za Taifa, na maeneo mengine ya utalii nchi nzima.
“Nimekuwa nikiripoti juu ya suala hili kwa miaka sita mfululizo, lakini hakuna jitihada za kuridhisha zilizochukuliwa na Serikali kulishughulikia.
“Pamoja na kuripoti mara kwa mara juu ya changamoto ya mimea vamizi katika miaka mitano mfululizo, niliendelea kubaini kuendelea kwa changamoto hiyo”ameeleza CAG Kichere.
CAG Kichere amebainisha kuwa katika tathmini yake ya utendakazi ya Mwaka wa Fedha 2024/25 kutoka kwenye hifadhi 11 amebainisha kuwa mimea vamizi hushughulikiwa pale tu inapoonekana imezidi badala ya kuchukua hatua stahiki ili kuweza kuizuia.
Aidha ameongeza kuwa Hifadhi za Taifa zinazingatia hatua za kienyeji kama vile kukata na kuchoma moto badala ya kutumia mbinu za kisayansi ili kuzuia.
Amefafanuwa kuwa Mamlaka ya Hifadhi ya Taifa ilieleza kuwa inaandaa Mpango wa Usimamizi wa Mimea Vamizi ambao utajumuisha hatua mbalimbali za kinga kama vile vituo vya magari ya kupuliza kwenye mageti ya kimkakati ya hifadhi.
Aidha amebainisha kuwa Mamlaka ilieleza kuwa, kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania, na taasisi husika za mafunzo, inapanga kukusanya rasilimalifedha ili kuweza kukabiliana na tatizo.
“Ninaamini kuwa juhudi zilizotajwa zitasaidia kuzuia mimea vamizi, urejeshaji wa uhifadhi, na programu za uhamasishaji wa umma, hivyo kuimarisha usimamizi wa mazingira na usimamizi endelevu wa hifadhi.
“Ninarudia mapendekezo yangu kuwa: (a) Serikali itangaze suala la mimea vamizi kuwa tatizo la kitaifa na ihakikishe wadau wa ngazi zote wanahusishwa ili kuchukua hatua za kuondoa, kudhibiti na kuzuia kuwapo kwake ndani ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, katika hifadhi zingine za taifa, na katika maeneo mengine kote nchini;
“Mamlaka ya Hifadhi za Taifa Tanzania iharakishe mchakato wa kuandaa programu ya usimamizi wa mimea vamizi, huku ikishirikisha na wadau wengine muhimu, kisha ihakikishe inatekelezwa kwa ukamilifu katika ngazi ya Kitaifa”ameeleza CAG Kichere
CAG Kichere pia katika ripoti yake ya Mwaka Fedha 2023/24 Kwa Mashirika ya Umma ameendelea kueleza juu ya kusambaa na kuongezeka kwa Kasi kwa Mimea Vamizi Zaidi ya Uwezo wa Hifadhi Kudhibiti
Amesema licha ya kuripoti kwa miaka mitano mfululizo kuhusiana na mimea vamizi, suala hilo bado halijatatuliwa kutokana na kutokuwepo kwa hatua za kutosha za kukabiliana na hali hiyo.
Ameongeza kuwa katika mwaka wa fedha 2022/23 Mamlaka ya Hifadhi za Taifa ilipanga kung’oa na kuondoa mimea vamizi kutoka katika hekta zipatazo 3,384.22 katika Hifadhi 15, hata hivyo, Mamlaka ilifanikiwa kung’oa na kuondoa katika hekta 2,352.53 tu ya lengo lililopangwa (sawa na asilimia 69.50).
Aidha ameeleza kuwa Mamlaka ya Hifadhi za Taifa ilifanya utafiti kwenye hifadhi nyingine mbili za Kilimanjaro na Burigi-Chato na kubaini hekta 507.01 zilikuwa zimeathirika na mimea vamizi.
“Huku mwaka wa fedha 2023/24 Mamlaka ililenga kungóa na kundoa mimea vamizi kutoka katika hekta zipatazo 16,734.3 lakini iliweza kungóa hekta 1,311.26 tu (sawa na asilimia 18 ya lengo), na kuacha hekta 15,423.04 (sawa na asilimia 72).
“Mimea vamizi huhatarisha mifumo ya ikolojia ya hifadhi kwani baadhi ni sumu, huondoa mimea asilia na malisho na pia mimea vamizi hailiwi na wanyamapori.
“Kwa hiyo, ninarudia pendekezo langu kuwa Serikali kutangaza tatizo la mimea vamizi kuwa suala la kitaifa na kuhakikisha wadau wa ngazi zote wanahusishwa ili kuchukua hatua za kuondoa, kudhibiti na kuzuia kuwapo kwa mimea hiyo ndani ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, katika hifadhi zingine za taifa, na katika maeneo mengine kote nchini”ameongeza CAG Kichere
Hata hivyo katika ripoti yake ya Mwaka wa Fedha 2022/2023 kwa Mashirika ya Umma, CAG Kichere ameeleza juu ya kusambaa na kuongezeka kwa mimea vamizi zaidi ya uwezo wa hifadhi kuyadhibiti
Katika ripoti hiyo,CAG Kichere amebainisha kuwa amekuwa akitoa taarifa juu ya hali mbaya ya kuenea kwa mimea vamizi na alipendekeza kuwa Serikali ifikirie kutangaza tatizo la mimea vamizi kuwa suala la kitaifa na kuhakikisha wadau katika ngazi zote wanahusishwa ili kuchukua hatua stahiki katika kuondoa, kudhibiti na kuzuia kuwapo kwa mimea hiyo ndani ya Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, kwenye Hifadhi za Taifa, na katika maeneo mengine nchini.
“Nimekuwa nikiripoti juu ya suala hili katika miaka minne mfululizo ya fedha, lakini hakuna jitihada kubwa zilizochukuliwa na Serikali kulishughulikia tatizo hilo”amesema CAG Kichere
Ukaguzi wangu wa 2022/23 umeendelea kubaini kuendelea kwa tatizo hilo,Kwa mfano, katika mwaka wa fedha 2022/23 Hifadhi ya Taifa ilipanga kung’oa na kuondoa magugu vamizi kwenye hekta za mraba zipatazo 3,384.22 katika Hifadhi za Taifa 15.
Hata hivyo, Mamlaka iliweza kung’oa hekta za mraba zipatazo 2,352.53 (asilimia 69.5) ya maeneo yaliyopangwa”amebainisha CAG Kichere
CAG Kichere ameongeza kuwa Hifadhi ya Taifa ilifanya utafiti kwenye hifadhi zingine mbili za Kilimanjaro na Burigi-Chato na kubaini Hekta 507.01 ambazo zimeathiriwa na magugu vamizi.
“Kwa hiyo, ninarudia pendekezo langu kuwa Serikali ifikirie kutangaza tatizo la mimea vamizi kuwa suala la kitaifa na kuhakikisha wadau wa ngazi zote wanahusishwa ili kuchukua hatua za kuondoa, kudhibiti na kuzuia kuwapo kwa mimea hiyo ndani ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro, katika hifadhi zingine za taifa, na katika maeneo mengine kote nchini”amebainisha CAG Kichere

Discussion about this post