NA MFAUME PASTORY,NJOMBE
MAMLAKA ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imewahimiza waandishi wa habari nchini kuwa mstari wa mbele katika kuisemea jamii kuhusu mambo yanayofanyika kinyume na utaratibu ili kuepusha madhara makubwa kutokea .
EWURA ambayo ni taasisi ya Serikali iliundwa mwaka 2001 kwa mujibu wa Sheria ya EWURA, Sura ya 414 ya Sheria za Tanzania na kuanza kazi Septemba 2006.
Madhumuni ya kuundwa EWURA ni kufanya udhibiti wa huduma za nishati na maji kwenye nyanja za kiufundi na kiuchumi za sekta ya nisahti na maji na usafi wa mazingira.
Hata hivyo EWURA inayoongozwa na Mkurugenzi Mkuu wake Gerald Maganga,kwa mujibu wa Kifungu cha 7 cha Sheria hiyo,kinaeleza majukumu ya Mamlaka hiyo baadhi yake yakiwa ni pamoja na kutoa, kuhuisha na kufuta leseni,kuweka na kusimamia viwango vya ubora wa huduma,kudurusu na kusimamia bei za huduma
Majukumu mengine ya EWURA ni pamoja na kutunga sheria ndogo na kanuni na kufuatilia maendeleo ya sekta zinazodhibitiwa kwa kuzingatia upatikanaji, ubora wa huduma, gharama ya huduma, ufanisi wa uzalishaji, uwekezaji na usambazaji wa huduma.

EWURA ambayo imekuwa na utaratibu wa kutoa taarifa mara kwa mara kuhusu huduma za nishaji na maji kwa wadau wake mbalimbali ili kuwa na taarifa sahihi,imewahimiza pia waandishi wa habari,kuwa mstari wa mbele katika kuisemea jamii kuhusu mambo yanayofanyika kinyume na utaratibu ili kuepusha madhara makubwa kwa siku zijazo.
Wito huo umetolewa June 2,2026 mkoani Njombe na Meneja Mawasiliano wa Mamlaka hiyo Wilfredy Mwakalosi wakati ikiwasilisha mada ya Kazi na wajibu wa Ofisi ya EWURA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini katika mafunzo yaliyokuwa yakitolewa na Mamlaka hiyo kwa wanahabari ambao ni wanachama wa chama cha waandishi wa Habari Mkoa wa Njombe.
Mwakalosi amesema moja ya jukumu lao ni kuandaa na kuratibu mchakato wa kupata maoni ya wadau ambapo hapo ndipo eneo muhimu kwa wananchi kuelimishwa zaidi.
Aidha ameongeza kuwa waandishi wa habari wanapaswa kuwa sehemu ya kusaidia na kuisemea jamii pindi wanapoona mtu anayetaka kufanya uwekezaji lakini anakiuka taratibu za kisheria kabla hajaendelea na uwekezaji kwani baadae huwa si rahisi kumwambia aondoe uwekezaji huo.
“Waandishi wasaidie kutoa elimu na kutoa maoni, mnapaswa kuwa kimbelembele kuiwakilisha jamii, mfano yale malalamiko ambayo yalikuwa yakitolewa na wananchi kuhusu utitiri wa vituo vya mafuta ni kwa sababu wananchi walikua wanaona ila walikuwa hawezi kuchukua hatua za kuwasilisha malalamiko mahala husika kwa wakati”
“Hili ni eneo muhimu ambalo wananchi wanapaswa kulizingatia na kuwa na uwezo wa kuchukua hatua za mapema kutoa taarifa kwa mamlaka husika na changamoto hii huwa si tatizo la Mamlaka yetu ya EWURA kwani sisi niwasimamizi wa huduma inayotolewa”amesema Mwakalosi

Kwa upande wake Meneja wa EWURA Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Ndugu Walter Christopher amesema wananchi wanapaswa kuangalia umbali wa eneo la uwekezaji na chanzo kilipo kwani kwa wastani inapaswa kuwa umbali wa mita 30 na kuendelea ndipo watu wanapaswa kufanya uwekezaji.
“Hii ndio sababu EWURA inaendelea kujenga na kuimarisha mahusiano yake na wadau na wananchi ili iwe rahisi kufikiwa na kushughulika na kero zote za wananchi.
“Tumekuwa tukijenga mahusiano na wakuu wa wilaya kwa sababu wao wanafikishwa zaidi kero na wananchi na tumekuwa tukiwafikia wanahabari kwa kuwa ninyi mnauwezo mkubwa wa kuelimisha jamii ”ameeleza Christopher
Christopher amebainisha kuwa EWURA inazalisha machapisho ambayo huelezea mambo muhimu na inafanya hivyo ili jamii iwe na uelewa yakiwemo mambo mbalimbali ambayo EWURA imekwisha yashughulikia na kuyapatia utatuzi.

Akizungumzia kuhusu vyanzo vya maji, Christopher amefafanuwa kuwa mikoa ya kusini ina maji na maporomoka mengi ambayo chanzo chake kikuu cha nishati ya umeme imekuwa ni maji.
“Kanda nzima kwa sasa ina mafundi waliosajiliwa na EWURA zaidi ya 870 na kwa Mkoa wa Njombe pekee una mafundi zaidi ya 150.
“Tunawahimiza pia mafundi ambao wamekuwa na vipaji vya ufundi umeme ila hawajasomea basi wakajiendeleze Vyuo vya Ufundi Stadi (VETA) kwani Serikali imetoa fursa hiyo na kisha ,Mamlaka itawatambua na kuwapatia kibali cha kufanya kazi” ameongeza Christopher
Hata hivyo Christopher amewahimiza wananchi kuwatumia mafundi waliosomea na wenye vyetu vya EWURA ili kuepusha matatizo au majanga katika shughuli zao na makazi yao.
“Kutokana na utendaji bora wa EWURA imefanikiwa kupunguza kiwango kikubwa cha kupokea malalamiko.
“Kwa wastani sasa kwa mwezi tunaweza kupokea malalamiko mawili na yote yakashughulikiwa kwa ufanisi na pande zote husika zikaridhika kwa kuwa Mamlaka imekua ikihakikisha inatenda kwa usawa kwa wateja wake wote bila kuwa na upendeleo” amefafanuwa Christopher




Discussion about this post