NA GOODLUCK HONGO
UTAFITI wa Kilimo wa Mwaka 2022/23 Matokeo Muhimu uliotolewa Septemba 2025 na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) umeonesha kuwa Jumla ya tani Milioni 1.3 za ndizi zilizalishwa nchini Tanzania.
Kati ya kiasi hicho kilichozalishwa tani 1,352,281 zilizalishwa na kaya na tani 414 zilizalishwa kutoka mashamba makubwa ambapo Tanzania Bara ilizalisha tani 1,294,765 huku Zanzibar ikizalisha tani 57,516
Ripoti hiyo inatoa takwimu muhimu za kilimo kutoka kwa wakulima wadogo katika ngazi ya kaya na mashamba makubwa kwa lengo la kuarifu sera za serikali, mipango, na program katika ngazi ya kitaifa na kimkoa.
Ndizi pia ni moja ya zao la chakula kama yalivyo mazao mengine lakini pia zao la biashara kwa wakulima wadogo na wakubwa.
Hata hivyo baadhi ya mikoa inayolima ndizi ni pamoja na Mbeya,Morogoro,Kilimanjaro na Mkoa wa Kagera ambapo ndizi huzalishwa kwa wingi katika vijiji vya Mabira pamoja na Kamagambo katika Wilaya za Kyerwa na Karagwe.
Ndizi aina ya kali na kisukari na zingine ambazo kwa lugha ya Kabila la Wanyambo linalopatikana Wilaya ya Karagwe na Kyerwa huziita ebijoge na hutumika kutengeneza pombe inayojukana kama Rubisi na juisi yake inayojulikana kama togwa(Omulamba).
Ndizi hizo huvundikwa hadi zitakapoiva na kisha kumenywa na kuwekwa kwenye kifaa kinachoitwa Obwato.
Baada ya kuwekwa kwenye Obwato ndipo zinaaanza kusagwa (Kujuungwa) kwa kutumia miguu ikichanganywa na majani ili zisiteleze hadi zitakapoanza kutoa juisi inayojulikana kama Omulamba (togwa) bila kuchanganywa na kitu kingine chochote.
Omulamba (togwa) ikishapatikana itachujwa ili kuondoa makapi na kisha kurudishwa kwenye Obwato kama ilivyokuwa awali na hapo ndipo linaweza kuuzwa ili watu waweze kunywa kama togwa(Omulamba).
Togwa hilo baada ya kupatikana na kuwa tayari kutumika,hufuatia hatua za utengenezaji wa pombe inayojulikana kama Rubisi.
Kwa upande wa utengenezaji pombe hiyo ya Rubisi,huchukuliwa Omulamba(togwa) lililo tayari kutumika na kisha kuchanganywa na Mtama uliokaangwa na kusagwa unga wake ndipo huvundikwa tena kama ilivyokuwa kwenye upatikanaji wa togwa.
Mchanganyiko huo huvundikwa kwa muda wa siku tatu ikiwa kwenye Obwato na baada siku hizo ndio hutolewa na kisha kuchujwa kuondoa makapi na hapo ndipo pombe ya Rubisi inapopatikana.
Kutokana na mazingira ya utengenezaji wa juisi hiyo maarufu kama Omulamba kwa wakazi wa Kagera ulisababisha Mhadhiri Mstaafu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM)Prof.Oscar Kibazoi kuamua kufanya utafiti katika kutengeneza juisi isiyo na kemikali kwa kutumia ndizi zenye utomvu mkali.
Anasema kinywaji ni sehemu ya chakula na Tanzania bado inaagiza juisi kutoka nje ya nchi na pale wanapokunywa basi wanachangia kuzalisha ajira kutokana na uzalishaji kuongezeka.
Akizungumzia na waandishi wa habari hivi karibuni jijini Dar es Salaam sababu za kufanya utafiti huo miaka 20 iliyopita na kutoa matokeo yanayoweza kuzalisha makumi ya ajira kwa watanzania,Prof.Kibazoi anasema wakati alipomaliza Degree ya pili aliona jinsi togwa la ndizi linavyotengenezwa mkoani Kagera ambapo walitumia mikono na miguu.

Anasema mkoani Kagera watu wengi wanalima zao la ndizi ili wale na sio kwa ajili ya fursa kama hizo hivyo wao waliangalia pia jinsi ya kuongeza thamani zao la ndizi.
Anasema baada ya kukanyaga ndizi hizo ili zilainike ndipo hupatakana togwa ambalo likikaa siku tatu huzalisha pombe ya ndizi.
Anasema kilichosukuma zaidi kufanya utafiti ni suala la usafi baada ya kuona jinsi wanavyotumia miguu na mikono kutengeneza togwa na alifanya utafiti kwa muda wa miaka mitatu ikiwemo kujua ukakasi wa ndizi na utomvu wake na faida zake kwa mwili wa binadamu.
Anasema baada ya utafiti huo ndipo walianza kusaga ndizi kwa kutumia mashine ndogo na kisha kutengeneza togwa la juisi ya ndizi bila kutumia mikono wala miguu.
“Ili utengeneze togwa(juisi) ya ndizi ni lazima upate ndizi yenye utomvu mkali au mwingi sana hivyo bila kuwa na ndizi yenye utomvu mwingi huwezi kutengeneza juisi hiyo.
“Ndizi ina madini mengi sana ikiwemo madini ya chuma hivyo tuliona kutengeneza juisi ya ndizi itasaidia hata afya kwa watanzania.
“Na faida ya juisi hii ya ndizi kwanza inaondoa kiu,kupata madini,sukari ambapo hupunguza kiwango hicho hadi kufikia asilimia 13 na hii ni juisi ya asili isiyo na kemikali yoyote ndani yake”anabainisha Prof.Kibazoi
Aidha anaongeza kuwa juisi hiyo inaweza kukaa zaidi ya mwaka mmoja bila kuharibika ambapo kwa sasa hawajanza kuzalisha kwa ajili ya biashara lakini wapo katika kutafuta uwezeshwaji ili kufungua kiwanda kikubwa cha kuzalisha juisi ya ndizi.

Akizungumzia utafiti wake na Dira ya Maendeleo 2050,Prof.Kabazohi anasema teknolojia yao ya kutengeneza juisi ya ndizi inaendana na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2050 inayotaka kufikia uchumi wa Sh.Trilioni moja.
“Tanzania tunaagiza sana juisi kutoka nje lakini hii juisi ni sehemu ya chakula hivyo watu wanapokunywa kwa wingi basi inachangia ajira katika mfumo wa uzalishaji kwa wingi”anaeleza Prof.Kabazohi.
Akizungumzia kuhusu elimu ya amali,Prof. Kibazohi anasema ni muhimu kuzidisha mafunzo kwa vitendo hasa kwa elimu inayohusu uhandisi ananainisha kuwa:
“Kwa upande wa kemia na usindikaji,tungeweza kuwa na fedha tungeweza kuwa na viwanda vidogo vidogo na sio vya matunda au mbogamboga tu hata vya kutengeneza mbolea kwa sababu tuna gesi asilia.
“Elimu hizi tumezipokea kutoka nje zimeletwa,sasa utafiti wangu umejikita katika mambo ambayo yapo hapa hapa nchini kwetu ambayo yanafaa kuendelezwa.
“Ukienda kwa mzungu ukimwambia hii ni juisi ya ndizi atashangaa sana,ingawa taratibu za sayansi au uhandisi ni zile zile; nadhani kuna haja ya kuangalia tunachomekaje masuala ya kwetu katika zile elimu”anaongeza Prof.Kibazoi

Prof.Kibazoi anabainisha kuwa watu wakitoka pale waende pamoja na mazoezi kuendeleza vya kwetu kwa sababu bila kuweka mle ndani na kuwafundisha tu kutoka nje hawana mahali pa kuviendelezea.
“Tunaweza tukaweka mitaala ambayo inaangalia huko na sio kununua mbolea kutoka nje na Serikali ikafadhili kununua mitambo ya kuendeleza na kuelekea huko na waanze kuwa wajasiriamali wa kutengeneza bidhaa. zinazotokana na malighafi zinazopatikana hapa nchini”anaongeza Prof.Kibazoi
Akizungumzia kuhusu uzalishaji wa ajira,Prof….anasema unaweza kuanza na ajira ya watu 10 kwa ajili ya uzalishaji na usambazaji lakini soko likiwa kubwa na ajira zitaongezeka zikiwemo za madereva,shambani na baadaye unaweza kufika hata watu 100.
“Mwanasheria au Mwandishi wa habari anapomaliza shule yeye anataka printa na kompyuta mapakato(laptop) tayari yupo kazini lakini Mwanasayansi na Mhandisi yeye anahitaji mitambo na wakati fulani tulifikiria kuwa na kiwanda kinachofanya kazi vizuri na tuligundua kuwa tunahitaji mitambo yenye gharama siyo chini na Sh.Bilioni moja na zaidi
“Lakini tumefupisha hapa kwenye hii Bilioni moja angalau tupate mahali pa kuanzia kwa sababu gani,Bilioni moja haipo kwani ili uweze kumsimamisha mtoto mdogo aanze kutembea ni lazima kwanza awe anatambaa,kama hajaanza kutambaa huwezi kumshikilia asimame”anafafanuwa Prof.Kibazoi
Hata hivyo anabainisha kuwa wanahitaji fedha ili waanze kidogo kidogo katika hatua za uzalishaji ili mtoto atambae,asimame na ndipo awepo mtu wa kumfundisha kukimbia.
“Benki hawataki kesho wapate hasara,sio wamshikilie mtoto ambaye hajaanza kutambaa wanataka kumfundisha kutembea aanguke,wao wanataka kuona kwamba je mmeshaanza kuzalisha,unazalishaje,soko lako likoje hela zipo lakini mwanzoni lazima tubebwe bwebe kidogo ili tuweze kufika mahali”anasema Prof Kibazoi
COSTECH yaongeza nguvu
Akizungumzia kuhusu kukamilisha utafiti wake,Prof.Kibazohi anasema walipata fedha ya awali na baadaye kupata fedha ya pili kutoka Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) kiasi cha Sh.Milioni 100 ambapo baadhi ya fedha hizo zilisaidia kukamilisha utengenezaji wa juisi hizo zinazoonekana tayari.
“Kilichopo sasa hivi ni kutaka tuingie katika uzalishaji ambapo tutahitaji sehemu ya kuzalishia,mashine za kukamulia juisi,wataalam na baada ya hapo tutaengeneza na mvinyo na hata pombe na vitu vingine.
“Ili uweze kutengeneza mvinyo unahitaji tunda lenye sukari zaidi ya asilimia 19,sasa sisi tunapata mpaka asilimi 28 ya sukari na inategemea aina ya ndizi hivyo ni rahisi kutengeneza mvinyo.
“Mwekezaji anayehitaji kuja basi tunamkaribisha”anabainisha Prof.Kibazoi




Discussion about this post