BAJETI ya Wakala wa Barabara Vijijini (TARURA) imepanda kutoka Sh. Bilioni 25 hadi kufikia kiasi cha Sh.Bilioni 40 kwa Mkoa wa Dar es Salaam huku kitaifa ikifikia Sh.Bilioni 300.
Kauli hiyo imetolewa leo mkoani Dar es Salaam na Mkuu wa Mkoa Amos Makalla wakati wa utilianaji sahini awamu ya kwanza ya mikataba 41 yenye thamani ya Sh. Bilioni 14.1 kwa ajili ya ujenzi wa Barabara za Mkoa wa Dar es salaam.
Amesema anamshukuru na kumpongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza bajeti ya barabara za TARURA nchi nzima hali itakayosaidia uboreshwaji wa barabara za vijijini.
“Ninafurahishwa na ongezeko la bajeti ya Ujenzi wa Barabara Dar es salaam kutoka Sh. Bilioni 25 hadi Sh.Bilioni 40 na kwa nchi nzima kufikia Sh.Bilioni 300.
Makalla amesema mafanikio hayo yote ni matokeo ya kazi kubwa na nzuri ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan Katika utatuzi wa kero za wananchi.
Aidha RC Makalla amewaelekeza Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka (DAWASA),Wakala wa Barabara nchini(TANROADs), Wakala wa Barabara Vijijini(TARURA), Shirika la Mawasiliano Tanzania(TTCL) na Shirika la Umeme nchini(TANESCO) kufanya kazi kwa pamoja ili kuondoa tatizo la miradi kutomalizika kwa wakati Kutokana na taasisi husika kuchelewa kuhamisha miundombinu.
Hata hivyo Makalla amewaelekeza TANROADs na TARURA kuhakikisha wanasimamia utunzaji wa miundombinu ya barabara ikiwa ni pamoja na usafi, ukarabati na uwekaji wa vibao vya kuzuia biashara kwenye eneo la hifadhi ya barabara. Makalla amewahimiza wakandarasi wote waliosaini mikataba hiyo kuhakikisha wanakamilisha miradi kwa wakati na kwa viwango vinavyohitajika.
Discussion about this post