JESCA KIKYA,ARUSHA
WAZIRI wa Nishati January Makamba amesema maendeleo ya Sekta ya Mafuta na Gesi nchini yana dhamira ya kulisaidia Taifa kuanzia ngazi ya mapato hadi miradi ya kimkakati.
Kauli ya Makamba imekuja siku chache baada Rais Samia Suluhu Hassan mnamo Mei 11, 2022 kushuhudia utiaji saini wa makubaliano ya awali ya Mkataba wa Nchi Hodhi (HGA) wa Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia kuwa katika hali ya kimiminika (LNG).
Mkataba huo umesainiwa baina ya Serikali na makampuni ya Shell na Equinor ambao ndio wabia wakuu wa utekelezaji wa mradi huo wenye thamani ya Dola za Kimarekani Bilioni 30 sawa na Sh.Trilioni 70) unaotarajiwa kutekelezwa katika eneo la Likong’o mkoani Lindi.
Katika hafla hiyo iliyofanyika Ikulu Chamwino jijini Dodoma, Rais Samia amesema mradi huu ni mkubwa, wa kimkakati na mahususi kwani unaleta mtaji na mapato nchini.
Akizungumza leo jijini Arusha wakati akizindua Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC).Makamba amesema Bodi hiyo itachochea kasi ya ukuaji wa maendeleo katika shirika hilo.
Amefafanua kuwa maendeleo ya sekta ya nishati hizo nchini yapo katika dhamira ya kulisaidia Taifa kufikia kuweza kuleta mchango kwa serikali kuanzia ngazi ya mapato na miradi mikubwa ya kimkakati.
Aidha amebainisha kuwa ,uteuzi wa bodi hiyo una akisi dira na malengo mapya ya serikali kwa shirika hilo kuelekea katika mafuta na gesi.
“Bodi hii chini ya Mwenyekiti wake Balozi Ombeni Sefue inakidhi nafasi ya TPDC katika maendeleo ya nchi, dira na mwelekeo mpya wa TPDC katika uchumi mpya wa gesi na maendeleo ya mafuta nchini”amesema Makamba
Mwenyekiti wa Bodi hiyo ya TPDC Balozi Ombeni Sefue ambaye pia ni Katibu Mkuu Kiongozi Mstaafu amesema kazi yao ni kuhakikisha kila kitu kinakwenda kama inavyotakiwa na sekta hiyo ya Mafuta na Gesi ili Taifa liweze kunufaika na rasilimali hizo.
Awali Mkurugenzi wa TPDC Dkt James Matarajio amesema kuwa ,miradi ya mafuta na Gesi itakapokamilika itasaidia kutatua changamoto za wananchi.
“Tuna miradi mikubwa ya uchakataji wa Gesi Asilia ambao unatarajiwa kujengwa kwa viwanda na utagharimu Sh.Bilioni 40 ikiwemo pia mradi wa kujenga Bomba la mafuta kutoka Hoima nchini Uganda ambao umeonesha mafanikio tokea umeanza
“Pia kuna mradi wa kutafuta mafuta katika Bonde la Ufa ambao upo kwenye mchakato wa awamu ya kwanza ya uchimbaji”amefafanua Matarajio
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli,(PURA)Mhandisi Charles Sangweni amesema uundwaji wa bodi ya shirika hilo utasaidia kuleta tija na maendeleo katika mamlaka yao hususani upande wa maamuzi kwani imekaa muda mrefu bila kuwa na bodi.
“Taasisi yoyote isipokuwa na bodi inakuwa haijakamilika”amebainisha Sangweni
mwisho




Discussion about this post