LUSAKA ,ZAMBIA
ZAMBIA imesema itaanza ujenzi wa bomba la mafuta lenye urefu wa Km. 700 sawa na maili 435 ili kuingiza mafuta ya dizeli kutoka nchini.
Ujenzi huo ambao utafanyika kwa awamu tatu utagharimu dola za kimarekani Milioni 300 katika ujenzi wa awali.
Waziri wa Nishati wa Zambia Peter Kapala ametoa kauli hiyo Juni 3,2020 na kuongeza kwamba bomba hilo jipya litaenda sambamba na la sasa lakini litakuwa la kisasa zaidi.
“Baada ya miezi michache, bomba litaanza kusukuma mafuta ya dizeli nchini Zambia kutoka Tanzania”amesema Kapala
Amesema awamu ya kwanza ya bomba hilo itaishia Mpika (Wilaya ya Kaskazini mwa Zambia), awamu ya pili Ndola (Mkoa wa Copperbelt) na awamu ya tatu Solwezi (kaskazini magharibi mwa Zambia),”
Hata hivyo,Kapala hakutoa maelezo zaidi kwa awamu ya pili na ya tatu ya mradi huo.
Ujenzi wa bomba hilo unakuja wakati ambapo Serikali kwa kushirikiana na nchi ya Zambia wanatumia bomba la mafuta la TAZAMA, lenye urefu wa Km 1,710 sawa na maili 1,063 kusafirisha mafuta ghafi ya petroli kutoka bandarini hadi katika Kiwanda cha Kusafisha Petroli cha Indeni kilichopo Ndola, Zambia.
Aidha Kapala amesema bomba la dizeli, ambalo litakuwa na ubora wa hali ya juu zaidi kuliko TAZAMA, litakuwa muhimu katika malengo ya muda mrefu ya nchi hiyo ya kuleta utulivu wa usambazaji wa dizeli ikiwemo kudumisha bei nzuri ya reja reja.
Matumizi ya sasa ya dizeli ya kila siku nchini Zambia yanakaribia lita milioni mbili, huku watumiaji wakuu wakiwa migodini, na kiwango cha usambazaji wa bidhaa nchini humo kimesalia kuwa salama licha ya changamoto za vita nchini Ukraine na Urusi.
mwisho




Discussion about this post