NA MWANDISHI WETU, Dodoma
WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki amesema Serikali itaajiri Maafisa Ugani zaidi ya 300 ili kupunguza changamoto ya uhaba wa wataalamu hao.
Mbali na hilo lakini pia watanunua pikipiki zaidi ya 1000 kwa ajili ya kuwawezesha maafisa hao kutekeleza majukumu yao kwa urahisi.
Ndaki ametoa kauli hiyo wakati akifungua mkutano wa wadau kutoka Sekta ya Mifugo uliofanyika jijini Dodoma jana.
Ndaki amesema kwa mwaka huu wa fedha serikali itatoa ajira hizo na kununua pikipiki hizo ili kuwasaidia kuwafikia kwa wakati wafugaji hasa wakati huu ambapo kutakuwa na kampeni kubwa ya kutoa elimu kwa wafugaji ili kufuga kisasa na kuchangia pato la Taifa.
Amesema wafugaji wengi nchini bado wanafuga kienyeji na kupelekea sekta ya mifugo kutokuwa na tija kubwa, hivyo ni wakati sasa watafiti wasaidie kutatua changamoto hiyo.
“Kama tutaendelea kufuga kama tunavyofuga leo kwa kuswaga Ng’ombe, baada ya miaka 10 ijayo tutaleta shida kwenye nchi hii, kwa sababu maeneo ya malisho yamepungua, hivyo watafiti watusaidie kuja na majibu yanayolenga kutatua changamoto hii, tuone namna gani tutakabiliana na jambo hili”, amesema Ndaki

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Wadau wa Sekta binafsi waliohudhuria Mkutano wa Wadau wa Mifugo uliofanyika jijini Dodoma Jana. Kulia kwake ni Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina.
Aidha amebainisha kuwa kwa mwaka huu wa fedha wao kama wizara wamejipanga kufanya kampeni kubwa ya kuwaelimisha wafugaji nchi nzima kuhusu ufugaji bora na wenye tija.
“Tutaanza kutoa elimu mwaka huu kuwaelimisha wafugaji kuhusu ufugaji bora na tutaendelea mpaka ujumbe huu wa kufuga kwa tija uwe umefika kwa wafugaji wote nchini”, ameeleza Ndaki
Aliendelea kusema kuwa Wizara imetenga bajeti kwa ajili ya kuelimisha wafugaji kuhusu malisho ya mifugo na mabadiliko ya tabia nchi ili wabadilike kutoka kufuga kiasili na kufanya ufugaji wa kibiashara.
Naye, Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Dkt. Charles Mhina amesema maendeleo ya Sekta ya Mifugo kwa kiasi kikubwa yanachangiwa na sekta binafsi.
“ Serikali itaendelea kuweka mazingira mazuri kwa wadau hao ili sekta hiyo iweze kuwa na mchango mkubwa katika pato la taifa”amesema Dkt.Mhina




Discussion about this post