NA MWANDISHI WETU
MKURUGENZI Msaidizi wa Watoto kutoka Wizara ya Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi Maalum Mathias Haule amesema wazazi wanajukumu kubwa la kuhakikisha usalama wa watoto unakuwepo.
Kauli ya Haule imekuja wakati ambao ongezeko la vitendo vya ukatili dhidi ya watoto vikiongezeka kwa kasi.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati wa kuanza kwa uundaji wa mabaraza na madawati ya watoto shuleni kwa kuwahusisha maofisa Ustawi wa Jamii kutoka Mkoa wa Dar es Salaam kwa kushirikiana na Sos Children’s Villages,Haule amesema jukumu la kulinda usalama na kupinga ukatili dhidi ya watoto ni kila mzazi
Mkutano huo ambao umewashirikisha wadau na mashirika ya kupinga ukatili dhidi ya watoto umekuja siku chache baada ya kuzinduliwa kwa Mwongozo mpya wa Taifa wa Uundaji na Uendeshaji wa Mabaraza ya Watoto Tanzania jijini Dodoma.
Alisema Serikali inaendelea kupokea maoni ya wadau na kuyafanyia kazi katika kuhakikisha kuwa watoto wanalindwa dhidi ya ukatili.
Alisema wao kama Wizara wamewezesha kuanzishwa kwa madawati na mabaraza ya watoto lakini jukumu la kuimarisha ulinzi wa watoto ni la kila mtanzania.

Mratibu wa Mradi wa Kuimarisha Familia kutoka Sos Children’s Villages Kennedy Mshema akizungumza na Maofisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Dar es Salaam wakati wa uundaji wa mabaraza na madawati ya watoto shuleni uliofanyika jana jijini Dar es Salaam (Picha na mpigapicha wetu)
Kwa upande wake Mratibu wa Mradi wa Kuimarisha Familia kutoka Sos Children’s Villages Kennedy Mshema alisema wao wamekuwa na miradi mbalimbali ikiwemo kuwakutanisha wadau ili kuhakikisha kuwa ushiriki wa watoto katika kutambua haki zao pamoja na ulinzi ili kuondoa ukatili dhidi yao.
“Sisi SoS Children’s Villages kwa kushirikiana na Serikali kupitia Mkoa wa Dar es Salaam tumeanza uundwaji wa mabaraza ya watoto na madawati ya watoto shuleni.
“Tumewezesha wanafunzi kushiriki kikamilifu siku ya Mtoto wa Afrika ikiwemo kuzishirikisha shule za Zingiziwa na Chakina kama shule za mfano katika juhudi za kupinga ukatili dhidi ya watoto”alisema Mashema.
Kwa upande wake Mwanafunzi wa darasa la saba kutoka Shule ya Msingi Mjimwema iliyopo Kigamboni jijini Dar es Salaam Jovitha Joel alisema katika mkutano huo yeye kama mwanafunzi amejifunza mambo mengi ikiwemo kujua ukatili dhidi ya watoto.
“Nilikuwa sijui lakini sasa najua ukatili ni nini na nitaenda kutoa elimu hii kwa wanafunzi wenzangu na jamii inayonizunguka”alisema Joel




Discussion about this post