NA MIRIAM SARAKIKYA, ARUSHA
SERIKALI imetenga bajeti ya zaidi ya Sh. Bilioni 600 katika Wizara ya Maliasili na Utalii ambapo pamoja na kutumika katika maeneo mengine lakini pia baadhi ya fedha hizo zitatumika kutunza na kuhifadhi sehemu za historia na Male Kale nchini.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Maliasili na Utalii Balozi Dkt. Pindi Chana wakati akifungua mkutano wa nane wa Jumuiya ya Wataalamu na Watafiti wa Mambo ya Kale uliofanyika mkoani Arusha jana.
Waziri Dkt.Chana amesema Tanzania ina hazina ya historia ya masuala ya masalia ya Mali kale na kuna tafiti na taarifa mbalimbali za masalia ya Mali kale katika maeneo tofauti nchini ikiwemo Olduvai Gorge huku wataalamu wakiendelea kuvumbua masalia mbalimbali ya Mali kale .
Amebainisha suala la Mali Kale ni moja ya vipaumbele ambavyo kwa sasa wanaendelea kuvionyesha kwa watu duniani kote na kuendelea kutoa mwaliko kwa watalii kuja Tanzania kuona maeneo ya utalii wa utamaduni ikiwemo Mali kale
Kwa upande wake Mkufunzi wa Chuo Kikuu Cha Indiana nchini Marekani Prof. Jackson Njau ameeleza namna Jumuiya hiyo ya Wataaluma wa Mambo ya Kale ya Jiolojia wanavyofanya tafiti zao katika Bonde la Ufa kuanzia Ethiopia,Kenya na Tanzania
Aidha Prof. Njau amebainisha kuwa Jumuiya hiyo iliyoanzishwa na wanasayansi wenye asili ya afrika mnamo mwa 2007 kwa lengo la kuwaleta pamoja watafiti ,wahifadhi ,walimu wanafunzi na wasimamizi na watunga sera katika taaluma za akiolojia ,na jiolojia katika bonde la ufa.
Ameongeza kuwa lengo la kuwaleta pamoja ni waweze kujumuika na kubadilishana mawazo ikiwemo kushirikiana katika teknolojia mpya ya fani za Mali kale .




Discussion about this post