NA MIRIAM SARAKIKYA,ARUSHA.
WAZIRI wa Maji Jumaa Aweso amewataka wakuu wa mabonde ya maji nchini kulinda vyanzo vyao vya rasilimali hiyo ikiwemo kuweka mipaka ili visivamiwe na wananchi.
Aweso ameyasema hayo leo Agosti 26,2022 wilayani Arumeru katika Jiji la Arusha wakati akizindua Mradi wa Kuondoa Mchanga katika Mto Nduruma ili urejee katika mkondo wake wa asili.
Amesema ni muhimu kwa wakuu hao wa mabonde kushirikisha taasisi nyingine katika kulinda na kutunza vyanzo vya maji ikiwa ni pamoja na kuweka mipaka.
Aweso amefafanuwa kuwa kulinda na kuweka mipaka itasaidia zaidi kulinda vyanzo hivyo vya maji na sio kuathiri mazao ya wananchi pindi wanapotumia vyanzo hivyo kwa shughuli za kibinadamu.
Hata hivyo Aweso amemuagiza Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuongeza Sh.Milioni 100 katika mradi huo ili kufanikisha kukamilika kwake.
Wakati huo huo Aweso amewaelekeza viongozi wa Bonde la Mto Pangani kutoa mifuko 100 ya saruji kwa ajili ya maendeleo ya wananchi katika Halmashauri ya Meru.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhandisi Richard Ruyango amewashukuru madiwani wa Halmashauri ya Meru kwa kuridhia kutoa Sh.Milioni 1,000,000 kwa kila kata ambazo zilianza kuondoa mchanga katika mkondo wa maji wa Mto Nduruma nakupunguza changamoto za wananchi.
Aidha amewaomba viongozi wa Bonde la Mto Pangani wanaotekeleza mradi huo kuweka mipaka katika mito ukiwemo mto huo ili wananchi waweze kuelewa na kuacha kufanya shughuli za kibinadamu kandokando ya mito.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Mto Pangani Segule Segule ambaye anatekeleza mradi huo amewashukuru wananchi pamoja na viongozi wa Serikali ambao wanashirikiana katika kutunza vyanzo vya maji.
Diwani wa Kata ya Shambaraiburka John Mollel amebainisha kuwa athari za mto huo zimekuwa zikisababisha madhara makubwa kwa wananch ikiwemo kupoteza maisha kutokana na mafuriko wakati wa Mvua.




Discussion about this post