NA MWANDISHI WETU, MWANZA
MIRADI ya kimkakati inayotekelezwa na Serikali jijini Mwanza itafungua fursa za kiuchumi ikiwemo Utalii katika Kanda ya Ziwa na kurahisisha upatikanaji wa huduma mbalimbali kwa jamii.
Hayo yamebainishwa Oktoba 16,2022 jijini Mwanza na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii,Mary Masanja wakati wa ziara ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipokuwa akikagua maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Kigongo- Busisi, ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) eneo la Fela na uzinduzi wa jengo la huduma ya macho katika Hospitali ya Bugando.
Miradi hiyo ya kimkakati itakayosaidia kukuza utalii kuwa ni ujenzi wa Daraja la Kigongo-Busisi, Reli ya Kisasa ya SGR, Meli na upanuzi wa Kiwanja cha Ndege cha Mwanza.
“Tunaamini Kanda ya Ziwa itakuwa ni kitovu mahususi cha utalii nchini pindi miradi hii ya kimkakati itakapokamilika”ameeleza Masanja.
Aidha amebainisha kuwa uwepo wa miradi hiyo utarahisisha usafiri kwa watalii wanaotembelea jiji hilo kutoka nchi za jirani na wakati huohuo wizara inaendelea kupanua wigo wa utalii kupitia utalii wa mikutano na utalii wa majini.
Hata hivyo Masanja amewataka wananchi kanda hiyo hususani jiji la Mwanza kuendelea kupanda miti ili kutunza mazingira, ambapo husaidia uwepo wa hali ya hewa nzuri na kuhifadhi vyanzo vya maji.
“Wizara ya Maliasili na Utalii ina mkakati wa kuhakikisha kila mwananchi anapanda miti miwili, hivyo imeanzisha vitalu vya miti ambayo itagawiwa kwa wananchi”amesema.
Katika hatua nyingine,Masanja amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kwa kufanya kazi kwa nguvu kuhakikisha miradi hiyo inasonga mbele.
“Tuko pamoja kuhakikisha Serikali inasonga mbele chini ya Rais Samia Suluhu Hassan” ameongeza. Masanja.
Ziara ya Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa inaendelea jijini Mwanza ambapo leo Oktoba 17, 2022 atatembelea Kisiwa cha Ukerewe,Gana na kukagua maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Mabasi Nyegezi.




Discussion about this post