NA MWANDISHI WETU,DODOMA
TANZANIA inatarajia kunufaika na mradi wenye thamani ya Sh.Bilioni 120 kwa ajili ya miradi ya uhifadhi wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi kutoka Mfuko wa Mazingira wa Dunia (GEF).
Hayo yametangazwa Februari 13, 2023 jijini Dodoma na Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Mary Maganga wakati akifungua warsha ya Wadau na Wataalamu wa Mazingira inayolenga kuainisha vipaumbele vya miradi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi inayosimamiwa na GEF.
Maganga amesema Tanzania ni nchi mnufaika kutoka GEF ambapo itapokea kiasi cha Sh.Bilioni 120 kwa ajili ya miradi ya mazingira na mabadiliko ya tabianchi na kuwashukuru washirika hao wa maendeleo kwa kuandaa mpango huo wa utoaji wa fedha hizo ambazo hadi sasa tayari zimekwishatolewa kwa awamu na kusema kuwa zitasaidia katika juhudi za kuimarisha uhifadhi na usimamizi wa mazingira nchini.
Aidha Maganga amewataka wadau na wataalamu hao kutumia vyema ujuzi na uzoefu walionao katika kuimarisha mapambano na changamoto za mazingira zilizopo kwa lengo la kuhakikisha maandalizi na utekelezaji wa miradi chini ya GEF- awamu ya nane inatekelezwa kwa wakati.
“Tanzania ni nchi mnufaika wa miradi ya GEF ambayo inafadhiliwa kupitia mikataba mbalimbali ya kimataifa, hivyo Ofisi ya Makamu wa Rais imeona umuhimu wa kuita wadau na wataalamu kutoka wizara na taasisi za kisekta kutoka mashirika mbalimbali ili kuweka mikakati ya pamoja na kufanikisha ajenda ya mazingira,” amesema Maganga.
Hata hivyo ametoa wito kwa wataalamu hao kuhakikisha wanafanya maandalizi ya haraka ya kuainisha maeneo ya kipaumbele ya miradi ya washirika wa maendeleo ili kuanza katika mwaka uliowekwa na kuikamilisha kwa wakati.
Kwa upande wake Mratibu wa GEF Kanda ya Afrika Ibrahima Sow amebainisha kuwa Tanzania imetengewa mgao huo wa fedha za mzunguko wa nane katika maeneo matatu ya mradi kwa kipindi cha miaka minne ijayo.
Sow ametaja maeneo hayo kuwa ni Mradi wa Usimamizi katika Maziwa Makuu na Mabonde ya Maji, fedha za kujenga uwezo kwa wataalamu wa miradi pamoja na usimamizi wa miradi katika nchi zinazoendelea.
Naye Mkurugenzi wa Mazingira Ofisi ya Makamu wa Rais Dkt. Andrew Komba amesema katika eneo la kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali na kuhimiza na kuhamasisha utunzaji wa mazingira.
Ameongeza kuwa mabadiliko ya tabianchi ni miongoni mwa matokeo ya kuongezeka kwa gesijoto duniani sambamba na uharibifu wa uoto asili na bioanuai, hivyo Serikali imeanzisha kampeni za upandaji miti ili kuhakikisha nchi inakabiliana na athari hizo.




Discussion about this post