NA MWANDISHI WETU,PWANI
WAZIRI Kivuli wa Miundombinu kutoka Chama cha ACT-Wazalendo Mhandisi Mohamedi Mtambo amesema ni muhimu kuwepo na uwazi katika utoaji wa kandarasi za ujenzi ikiwemo barabara ili wananchi waweze kujua fedha zilizotolewa na Rais zinatumika katika viwango vinavyohitajika.
Mhandisi Mtambo ametoa kauli hiyo Februari 14,2023 Mkuranga mkoani Pwani wakati akizungumza kuhusu miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini ikiwemo ya Soko,Barabara Vituo vya Afya na Zahanati.
Amesema kumekuwa na usiri kati ya mtoa kandarasi na mkandarasi hivyo kupelekea miradi hiyo kushindwa kusimamiwa vema na wananchi na kujengwa chini ya kiwango.
“Mimi kama Waziri Kivuli wa Miundominu ikiwemo Ujenzi, Barabara na Reli, kutoka Chama changu cha ACT-Wazalendo tunataka kuwepo na uwazi kati ya mtoa kandarasi na mkandarasi ili kujua kiwango cha fedha zitakazotumika katika ujenzi huo,aina ya barabara inayojengwa na viwango vyake kama ni lami basi ijulikane ni ya kiwango gani,lakini pia tenda itolewe eneo husika.
“Ufunguzi pia ufanyike eneo husika kwa kuwahusisha Viongozi wa Serikali za Mitaa,Diwani na wananchi jinsi mradi huo utakavyotekelezwa katika eneo lao au utapita katika eneo lao hali itakayosaidia wananchi kulinda na kufuatilia kwa ukaribu lakini sio tenda inatolewa eneo lingine na ujenzi unafanyika eneo lingine.
“Tungependa kuona mabango yote ya wakandarasi yaandikwe kwa lugha ya Kiswahili ili wananchi waelewe na kufuatilia kwa karibu”amesema Mhandisi Mtambo
Mtambo ambaye pia ni Katibu Mkuu wa chama hicho Mkoa wa Pwani ameongeza kuwa wao wanaamini kuwa Taifa la wote na maslahi kwa wote hivyo uwazi utasaidia uwajibikaji na sio wananchi kuona mkandarasi akifikisha vifaa vya ujenzi eneo la mradi bila kujua kitakachojengwa, gharama zake na viwango vitakavyotumika katika ujenzi.
“Mfano kama unajenga barabara ya Mbande hadi Mbagala sasa hapa kandarasi itangazwe kwa uwazi na waanchi na viongozi wa Mbagala pamoja na Chamanzi na Mbane wajue,lakini pia wajue gharama zake,viwango vya ujenzi huo na uzinduzi ufanyike maeneo yao ikiwemo bango la ujenzi kuandikwa kwa lugha ya Kiswahili na sio lugha ya kiingereza”ameongeza Mtambo
Mtambo amebainisha kuwa kwa kufanya hivyo kutawafanya wananchi kushiriki na kulinda miradi hiyo ikiwemo kukosoa pale wanapoona hapaendi sawa kulingana na uwazi waliopata hivyo kusaidia fedha zinazotolewa kwa ajili ya ujenzi kutumika inavyokusudiwa.




Discussion about this post