NA MWANDISHI WETU,TANGA
MWANAFUNZI wa Kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Chumbageni jijini Tanga Adinan Sadik ametengeneza redio na vifanya vingine vya kieletroniki ikiwemo helkopta ambayo inadaiwa kuwa iliruka baada ya kuwekwa mota.
Mwanafunzi huyo ambaye anaonekana kuwa Mtafiti na Mbunifu amebuni pia kifaa cha kieletroniki ambacho kitatumika kuchomea dawa za mbu na udi ambapo ubunifu huo umethibitishwa pia na Diwani wa Kata ya Chumbageni Ernest Kimaya.
Akizungumza na tovuti hii ya Bajeti,Sadick amesema yeye anaweza kutengeneza vitu vinavyotumika na binadamu lakini anahitaji kusaidiwa zaidi ili kufikia ndoto zake za kuwa mwanasayansi.
“Nimetengeneza redio mbili na zinashika vituo vyote na sijafundishwa na mtu hivyo naomba nisaidiwe ili niweze kufikia malengo yangu”amesema Sadik
Kwa upande wake Mwalimu wa Somo la Sayansi katika Shule hiyo Burhan Kumba amesema mwanafunzi huyo ana kipaji kikubwa cha kutengeneza vitu vya kieletroniki na kwamba ametengeneza redio inayoshika vituo mbalimbali kwa kutumia boxi na waya za kawaida.
“Sisi kama walimu tulifanya jitihada za kuhakikisha wadau wa Elimu Mkoa wa Tanga wanafahamu taarifa za kuwepo kwa mwanafunzi huyu na vitu anavyobuni na kuvitengeneza lakini hadi sasa bado hatujapa muendelezo wake tangu tulipofikisha taarifa hizi”amesema Kumba
Kumba amesema wao kama walimu wameona ana kipaji cha hali ya juu hivyo walipendekeza pia kupelekwa katika shule za ufundi ili aweze kuendeleza ubunifu na kipaji chake ambapo pia waliwashirikisha wazazi wake katika kumsaidia.
Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Chumbageni Ernest Kibaya amesema jitihada zinaendelea za kumsaidia mwanafunzi huyo ili aweze kufikia lengo lake na kusaidia wengine kutokana na kipaji chake.
Hata hivyo Tume ya Raifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imekuwa ikishindanisha wabuni wa kisayansi na kiteknolojia katika mashindano maarufu kama MAKISATU ambapo washindi mbalimbali hujipatia zawadi na kuendelezwa kwa bunifu zao.




Discussion about this post