NA MWANDISHI WETU,ZANZIBAR
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar,kimepongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Mwinyi,kwa maamuzi yake ya kupandisha viwango vya pencheni za wastaafu pamoja na za jamii kwa wazee wenye umri wa miaka 70.
Pongezi hizo zimetolewa na Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Itikadi na Uenezi CCM Zanzibar Khamis Mbeto Khamis mara tu baada ya Rais Dk.Mwinyi, kutangaza viwango hivyo katika maadhimisho ya siku ya wafanyakazi kitaifa yaliyofanyika Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Mbeto, amesema hatua hiyo ni ya kupongezwa na imeandika historia kubwa katika falsafa ya utawala bora kwani mara nyingi wananchi wanaostaafu wamekwa hawapewi kipaumbele.
Amesema matunda hayo yanatoka na utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020/2025 ambayo imetekelezwa kwa ufanisi mkubwa na kukuza uchumi ulitoa fursa ya kupatikana kwa fedha za kuimarisha miradi mbalimbali ya kijamii ikiwemo kuongeza pencheni hizo.
Ameongeza kuwa Dk.Mwinyi,ameendelea kuwa kiongozi mwenye maono,utu,huruma na mzalendo wa kweli katika kusimamia haki na kuimarisha maisha ya wananchi wa makundi mbalimbali nchini.
“Tunampongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Mwinyi, kwa maamuzi yake ya kuongeza kiwango cha pensheni kwa wastaafu waliotumikia nchi kwa uadilifu mkubwa.
“Hatua hii ni miongoni mwa mikakati,sera na vipaumbele vya CCM katika kuinua hali ya maisha ya wananchi wa makundi mbalimbali nchini.
“Maamuzi hayo ya kuongeza pensheni kwa wastaafu wa kima cha chini kwa asilimia 100 ambapo mstaafu aliyekuwa akipokea kiasi cha Sh. 90,000/= atapokea Sh. 180,000/= na kwa upande wa pensheni jamii imepanda kwa asilimia 150 kutoka Sh. 20,000/= hadi Sh. 50,000/= kwa Wazee wenye umri wa miaka 70 ambapo mabadiliko hayo ya pensheni yataanza katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 ” amesema Mbeto
Aidha ameeleza kuwa Dk.Mwinyi, mbali na kuongeza kiwango hicho cha pencheni pia ameahidi kuyafanyia kazi mapendekezo mbalimbali yaliyotolewa na Chama cha wafanyakazi Zanzibar.
Naye Katibu wa Kamati Maalum ya NEC,Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa CCM Zanzibar Khadija Salum Ali, ameongeza kuwa hatua hiyo ya Rais Dk.Mwinyi ya kuongeza pensheni inatakiwa kuenziwa kwa vitendo kwani imejenga faraja na hamasa kubwa kwa wastaafu mbalimbali nchini.




Discussion about this post