NA MWANDISHI WETU,SHINYANGA
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo amezindua miradi yenye thamani ya Sh. Milioni 520 ikiwemo uchimbaji wa visima viwili virefu vya maji pamoja na kukagua lambo la kukusanyia maji.
Miradi hiyo inatekelezwa kupitia Mradi wa Kukabiliana na Mabadiliko ya Tabianchi kwa Kutumia Mifumo Ikolojia Vijijini (EBARR) unaoratibiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais
Hata hivyo uchimbaji wa visima hivyo unajumuisha mfumo wa sola kwa ajili ya kuvuta maji, matanki ya kuhifadhi maji pamoja na mfumo wa umwagiliaji na wa matumizi ya wananchi ikiwemo lambo lenye uwezo wa kukusanya maji lita za ujazo 252,299 zitakazowagilia hekta 287 za mazao ya mbogamboga, kiwanda kidogo cha sabuni na kikundi cha uzalishaji uyoga.
Akizungumza kwa nyakati tofauti na wananchi Mei 6,2023 wa vijiji vilivyonufaika na mradi huo vya Melela, Magali na Mingo vilivyopo wilayani Kishapu Mkoa wa Shinyanga,Dk Jafo amesema kuwa Serikali ina nia ya dhati ya kuhakikisha wananchi katika maeneo yenye ukame wanapata mafanikio.
Amesema Serikali inapeleka miradi kwa wananchi ili kuwasaidia katika kupata fursa za kimaendeleo pamoja licha ya kuwepo kwa changamoto za mabadiliko ya tabiachi zinazochangia ukame.
“Ndugu zangu niwashukuru sana kwa kutekeleza hii miradi na niwaombe tuilinde asitokee mharibifu akaja kuharibu miundombinu tumsimfumbie macho, lakini pia ajenda yetu kuu tutunze mazingira, usipoyatunza na kuyashughulikia mazingira yatakushughulikia”, amesema Jafo.
Kutokana na hali hiyo hivyo, Dkt. Jafo amewapongeza viongozi katika wilaya hiyo kwa usimamizi mzuri wa miradi na kuhakikisha kuwa wananchi wanaponufaika nayo linakuwa ni jambo la heri.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Joseph Mkude ameishukuru Serikali kwa kuwapelekea wananchi wa wilaya hiyo mradi wa EBARR.
Amesema kuwa kuwepo kwa lambo hilo kutasaidia wananchi hao kuepukana na adha ya changamoto ya uhaba wa maji inayowakabili wananchi wa Kijiji cha kiloleli.
Aidha Mkude ameongeza kuwa mradi huo utakuwa wa manufaa makubwa kwa wananchi kwani utasaidia kuhifadhi mazingira katika eneo hilo ikiwa ni katika kuunga mkono jitihada za Serikali za kulinda mazingira.
Mradi wa EBARR unatekelezwa pia katika Wilaya ya Simanjiro (Manyara), Mvomero (Morogoro) na Kaskazini ‘A’ Unguja (Zanzibar) chini ya ufadhili wa Mfuko wa Mazingira wa Dunia chini ya Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa (UNEP)




Discussion about this post