GENEVA,USWISI
KILA ifikapo Mei 31 ya kila mwaka Dunia huadhimisha siku ya kupinga matumizi ya tumbaku ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani (WHO), limezitaka nchi kuacha kutoa ruzuku kwa kilimo cha tumbaku na badala yake kuunga mkono na kusaidia kilimo cha mazao endelevu yatakayoweza kulisha mamilioni ya watu wenye uhitaji wa chakula.
Katika ujumbe wake wa siku hii ya kupinga matumizi ya tumbaku alioutoa Mei 31,2023, na kutangazwa na tovuti ya Umoja wa Mataifa ya UN Kiswahili,Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus amesema tumbaku inawajibika kwa vifo milioni nane kila mwaka lakini bado serikali duniani kote zitatumia mamilioni ya dola kuunga mkono mashamba ya tumbaku.
Amesema watu duniani kote wanakabiliwa na njaa wakati ekari milioni 300 za dunia zinatumika kulima tumbaku.Ghebreyesus
“Ni wakati wa kubadili mwelekeo wa juhudi zetu na kujikita na kilimo ambacho kinastawisha siha yetu na mazingira yetu.”amesema Ghebreyesus
Amesema WHO inafanyakazi kwa karibu na mashirika mengi ya Umoja wa Mataifa likiwemo la Chakula na Kilimo (FAO) na la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) kuwasaidia wakulima kuhamia kwenye kilimo mbadala wa tumbaku
“kwa kuchagua kulima chakula badala ya tumbaku tutatoa kipaumbele kwa afya, kulinda mfumo wa maisha na kuimarisha uhakika wa chakula kwa wote.”amesema Ghebreyesus
Lengo la maadhimisho ya mwaka huu ni kuujulisha umma hatari za matumizi ya tumbaku, mwenendo wa biashara wa makampuni ya tumbaku, nini kinachofanywa na WHO kupambana na janga la tumbaku na nini watu duniani kote wanaweza kufanya ili kudai haki yao ya afya, maisha yenye afya na kuvilinda vizazi vijavyo.
Siku ya kupinga matumizi ya tumbaku duniani huadhimishwa kila mwaka Mei 31 na mwaka huu imebeka maudhui “Lima chakula sio Tumbaku”




Discussion about this post