NA MWANDISHI WETU
CHUO Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), kimesema kitawatumia wahitimu wake zaidi ya 50,000 walioko ndani na nje ya nchi ili kuboresha mitaala na mifumo yake itakayoendana na mahitaji ya soko ikiwemo fursa za kuajiri wengine na kujiajiri.
Taasisi hiyo ya elimu ya juu nchini, ambayo ni ya tatu kuanzishwa baada ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine(SUA) cha mkoani Morogoro, imejipanga kuwa kitovu cha elimu inayokwenda na wakati.
Hayo yameelezwa Juni 13,2023 jijini Dar es Salaam na Makamu Mkuu wa chuo hicho (VC), Prof. Elifas Bisanda wakati akizungumza na waandishi wa habari katika Ofisi za Makao Makuu ya chuo hicho.
Amesema kupitia Mradi wa Mageuzi ya Elimu ya Juu Kiuchumi (HEET), ambao unafadhiliwa na Benki na Dunia, OUT wameamua kuwatafuta wahitimu wote (Alumni) na kupata maoni yao ya kuboresha utoaji wa elimu chuoni hapo.
“Tumeanza kutoa wahitimu wa kwanza mwaka 1999, hadi sasa tuna zaidi ya wahitimu 50,000 kila mahali, lakini tangu tuanze kutoa wahitimu hadi sasa mambo mengi yamebadilika katika dunia.
“Leo tunazungumzia mapinduzi ya nne ya viwanda, ambayo yametawaliwa na akili bandia yaani ‘Artificial Intelligence’ hivyo lazima tukae chini kama wanataaluma, tuone namna bora ya kuendana na mabadiliko haya kwa manufaa ya mhitimu, jamii inayomzunguka na taifa,” amesema Prof.Bisanda.
Prof.Bisanda amebainisha kuwa wameona uhitaji wa kuboresha mitaala na program zao, kutokana na uhalisia uliopo, kwamba mitaani kumejaa wahitimu ambao hawana uwezo wa kufanya kwa vitendo waliyoyasoma darasani lakini wanasubiri kuajiriwa.
Aidha ameongeza kuwa hiyo ndio sababu wanataka kuwafikia wahitimu wa OUT na waajiri ambao wameajiri wahitimu wa chuo hicho, ili kupata maoni yao katika maeneo yote yanayohusiana na kumwandaa mwanafunzi au mwajiriwa kulingana na mazingira ya sasa.
“Tunawaita wanafunzi wetu wa zamani, watupe maoni yao juu ya wapi na kipi tuboreshe, wapi na eneo gani tupunguze, kipi tuondoe, kwa sababu hakuna maana ya sisi tuendelee kutoa programu ambazo mhitimu akimaliza, haajiriki wala hawezi kuajiri wengine,” ameeleza Prof.Bisanda.
Prof. Bisanda ametolea mfano mabadiliko ya nyakati katika programu ya uhasibu, ambayo awali ilihusisha utunzaji wa vitabu vya hesabu na utunzaji wa fedha katika makabati, taaluma ambayo sasa inahitaji mifumo ya kidigitali isiyohitaji vitabu na droo za kutunzia fedha.
Mmoja wa wahitimu wa chuo hicho, Edius Marcel, amesema tayari amekamilisha kujaza utafiti huo na kuwataka wahitimu wenzake ndani na nje ya nchi, kuharakisha jukumu hilo ili kusaidia katika kujenga taasisi imara itakayowaandaa vizuri wanafunzi wa sasa na wa wakati ujao.
OUT kupitia mradi wa HEET, inajenga maabara saba za kisasa za sayansi katika mgawanyo wa kanda nchini,kuwajengea uwezo wahadhiri na wakufunzi wake ikiwemo kuboresha mitaala na kufanya mapitio ya mifumo yake iendane na mahitaji ya wakati.




Discussion about this post