NA MWANDISHI WETU
CHAMA Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimewavua uanachama wanachama wake sita kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo kutoa nje siri za chama hicho.
Mbali na hilo sababu nyingine iliyokifanya chama hicho kuwavua uanachama ni pamoja na kutumia mali za chama kwa manufaa binafsi pamoja na kupinga maazimio na misimamo ya chama nje ya vikao halali vya chama.
Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam,Mwenyekiti wa CHADEMA Kata ya Chanika Manispaa ya Ilala Ibrahim Ally amesema Kamati Tendaji ya Kata hiyo imefikia maamuzi hayo baada ya kujiridhisha pasipo shaka kuwa makosa hayo yanawakosesha sifa za kuendelea kuwa wanachama kwa mujibu wa katiba ya chama hicho.
“Kuanzia leo Oktoba 22,2023 waliovuliwa uanachama ni pamoja na Charles Sangiwa,Paul Kigonti,Augustino Mkello,Seif Haji,Ally Kakwaya na Frank Mwambepo.
“Wanachama hao hawaruhusiwi kujishughulisha na kazi za chama wala kutumia nembo yake mahali popote kwani kwa kufanya hivyo watakuwa wamekiuka sheria za nchi”amesema Ally
Aidha Ally ameongeza kuwa wanachama hao waliofukuzwa wamekuwa wakifungua ofisi ya chama hicho katika kata hiyo bila viongozi wao kujua ikiwemo kushawishi migomo ndani ya chama hicho .
“Wamekuwa wakiunda Kamati Tendaji ya Kata na kufanya vikao huku wakijua ni kinyume cha Katiba ya chama hivyo baada ya kupitia kwa kina tuhumu hizo na nyingine Kamati Tendaji ilikaa kikao chake Oktoba 21,2023 na kisha kuwaandikia barua ili waje wajieleze lakini hawakuja”amebainisha Ally
Kwa upande wake Katibu wa chama hicho Kata ya Chanika Arthur Calleb amesema mbali na kuwafukuza lakini pia taarifa hizo zimepelekwa katika Ofisi ya Jimbo,Wilaya na Ofisi ya Katibu Mkuu Taifa.
“Ikiwa wataendelea kufanya shughuli za chama basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao kwa kuwa hawa sio wanachama wetu tena hivyo kutumia nembo na jina la chama kwa manufaa yao binafsi wakati hawatambuliki litakuwa ni kosa”amesema Calleb




Discussion about this post