NA MWANDISHI WETU,ZANZIBAR.
KATIBU wa Kamati ya NEC,Idara ya Itikadi,Uenezi na Mafunzo wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar Khamis Mbeto Khamis amesema Chama cha ACT-Wazalendo hakina hati miliki ya Zanzibar na ikiwa wajitoa katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) basi nafasi yao itachukuliwa na vyama vingine
Amesema ACT-Wazalendo wanatakiwa kujua kuwa CCM na Serikali zake hazitishwi na yeyote iwe mtu,Chama cha kisiasa,kundi,taasisi ya ndani na nje ya nchi na ikiwa watajitoa basi nchi itaendeleza kubaki salama ikiongiozwa na CCM.
Hayo ameyasema Machi 17,2024 visiwani Zanzibar wakati akitoa ufafanuzi juu ya hoja mbalimbali kwa waandishi wa habari waliofika ofisini kwake Kisiwandui.
Amesema Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) haikuundwa kwa matakwa,hisani na ridhaa ya Chama kimoja cha ACT-Wazalendo bali ipo kwa matakwa ya Wananchi waliopiga kura ya maoni ya kukubali wote kupitia kura ya maoni na kwamba hata kujitoa katika Serikali hiyo unafuatwa mfumo ule ule wa kupiga kura ya maoni.
Ameongeza kuwa madai ya ACT-Wazalendo ya kujitoa katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) hayana mashiko kwani Serikali hiyo imeundwa kwa nguvu ya kura ya maoni ya Wananchi wote kupitia mabadiliko ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya Mwaka 1984.
Mbeto,amefafanua kuwa ACT-Wazalendo wana ajenda binafsi ya kuirejesha Zanzibar katika machafuko ya kisiasa kutokana na vitendo na kauli zao hizo za vitisho dhidi ya Serikali iliyopo madarani.
”Kama dhamira ya kujitoa katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa itatimia litakuwa sio jambo jipya kwani walishawahi kususia vikao vya Baraza la Wawakilishi na Uchaguzi wa marudio mwaka 2016 na nchi ilipiga hatua kubwa za kimaendeleo bila uwepo wao.
“Kwanza nataka ACT-Wazalendo wajue kuwa CCM na Serikali zake hazitishwi na yeyote iwe mtu,Chama cha kisiasa,kundi,taasisi ya ndani na nje ya nchi tupo imara hivyo waweke maneno ya akiba wasije kujuta juu ya maamuzi yao ya kukurupuka na mihemko ya kisiasa.
”Wajitoe tu vyama vipo vingi wengine watachukua nafasi yao wasijione wao ndiyo wenye hati miliki ya Zanzibar na nchi itaendeleza kubaki salama na CCM kuendelea kuwa Chama Tawala”amesema Khamis.
Akizungumzia juu ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Hussein Ally Mwinyi, ya kuwaita viongozi wa chama hicho kuzungumza nao,Khamis amebainisha kuwa hilo ni jambo la kawaida kwa Rais wa nchi kukutana na watu mbali mbali kusikiliza maoni yao kisha yeye ndo mwenye maamuzi ya kutekeleza kile anachoona kinafaa.
”Vikao vya Rais wa Zanzibar na ACT-Wazalendo vilikuwa vya maridhiano havina uhalali wa kisheria wa kumlazimisha Rais Dk.Mwinyi atekeleze matakwa yao na kwamba kama ipo nyaraka yoyote yenye saini za makubaliano ya pande zote mbili basi zitolewe hadharani kama wanavyotoa madai yao mengine.
”CCM ipo tayari kukaa mezani kusikiliza maoni,ushauri na hoja za Chama chochote cha kisiasa chenye ushauri mzuri wa kuimarisha masuala mbalimbali ya kijamii,kisiasa na kiuchumi”ameongeza Khamis




Discussion about this post