NA MWANDISHI WETU,ZANZIBAR.
KATIBU Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Balozi Dk. Emmanuel John Nchimbi amesema uwepo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar (SUK)umeondoa hali ya siasa za chuki na uhasama mkubwa uliokuwepo kabla ya kufikiwa kwa uamuzi wa kuundwa kwake,
Amesema uamuzi wa kuwepo kwa Serikali hiyo ulizingatia kutanguliza mbele usalama wa maisha ya watu kuliko maslahi ya vyama vya siasa na kwamba CCM itaendelea kutimiza wajibu wake wa kuongoza kwa misingi ya haki na uwajibikaji ili kudumisha umoja na utulivu nchini.
Balozi Dk. Nchimbi amesema hayo Machi 25,2024 wakati akizungumza na Wazee wa Mikoa minne ya CCM Kichama ya Unguja ikiwa ni siku ya pili akiwa kwenye ziara ya kikazi, akitokea Pemba.
Ameongeza kwa SUK ilikuwa kwa ajili ya usalama wa maisha ya watu, usalama wa Wazanzibar, usalama wa Watanzania kwani maisha ya watu ni muhimu kuliko kitu chochote na waliweka mbele maslahi ya nchi, utulivu na umoja wao na si vyama vya siasa.
“Mnakumbuka wakati fulani nikiwa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kila siku nenda rudi kwa helkopita kuja Zanzibar. Tulikuwa tunahangaika kuondosha uhasama na chuki. Najua kuna wakati wenzetu wanapata gadhabu na kuzungumza kwa jazba lakini tuendelee kuwavumilia.
‘’Sisi wana CCM tusiende huko hata kidogo. sisi ndiyo Chama tawala sisi ni walezi na mlezi hasusi,tusiache wajibu wetu wa kulea hata kidogo na kwamba mtoto ndiye anasusa. na katika hili naomba sana wazee wote wa Zanzibar na Tanzania, mniunge mkono,” amesema Balozi Dk. Nchimbi.
Aidha, Balozi Dk. Nchimbi pia amesisitiza msimamo wa CCM kuendeleza kutimiza wajibu wa kipekee wa kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar na misingi yake, akisema kuwa ndiyo yaliyowaweka watu wote kuwa sawa mbele ya sheria na kuondoa kila aina ya ubaguzi, ukiwemo wa matabaka, rangi na hali ya mtu.
“Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar yameondoa matabaka yakaleta utu, sote tunaunganishwa na utu wetu, tunao wajibu wa kipekee kuhakikisha tunaendelea kulinda misingi ya Mapinduzi.
‘’Tuko tayari kuendelea kuyalinda hakuna umbo au rangi au hali inampatia haki zaidi mtu mwingine kuliko mwingine na ukifanya ubaguzi wa namna hiyo wewe ni kaburu tena ukaburu hauna rangi”,alieleza Dkt.Nchimbi.
Naye Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa,amesema CCM inajivunia kwa kuwa na hazina ya Wazee wenye uzalendo,busara,hekima na uwezo wa kushauri mambo mambo mbalimbali yenye manufaa kwa maendeleo ya Chama na Serikali zake kwa ujumla.
Awali Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa CCM Zanzibar Hadija Jabir,aliwasihi Wazee hao kuendeleza utamaduni wa kukosoa,kushauri na kutoa maoni ya kuimarisha CCM pale wanapoona kuna mambo yanaenda kinyume na misingi ya kuanzishwa kwa Chama hicho.



Discussion about this post