NA MWANDISHI WETU
UTAFITI wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa Mwaka 2022 (DHS-MIS 2022) umebaini kuwa zaidi ya robo ya kaya za Tanzania zinamiliki baiskeli, ikilinganishwa na asilimia tatu zinazomiliki gari/malori.
Utafiti huo uliotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) umeonesha kuwa asilimia 53 za kaya Tanzania zinamiliki ardhi kwa ajili ya kilimo ambapo asilimia 54 ya kaya za Tanzania Bara na asilimia 20 ya kaya za Zanzibar zina miliki ardhi kwa ajili ya kilimo.
‘’Zaidi ya robo (27%) ya kaya za Tanzania zinamiliki baiskeli, ikilinganishwa na asilimia 12 za kaya zinazomiliki pikipiki na asilimia 3 za kaya zinazomiliki gari/malori.
‘’Asilimia 53 za kaya Tanzania zinamiliki ardhi kwa ajili ya kilimo ambapo 54% ya kaya za Tanzania Bara na 20% ya kaya za Zanzibar zina miliki ardhi kwa ajili ya kilimo’’umeeleza utafiti huo
Aidha utafiti huo umefafanua kuwa Kaya za Tanzania zina wastani wa watu 4.5 ambapo asilimia 29 ya kaya hizo zinaongozwa na wanawake ambapo takribani nusu sawa na asilimia 46 ya watu wote katika kaya hizo ni watoto wa umri chini ya miaka 15.
Awali akizungumzia utafiti huo Machi,13,2024 mkoani Dar es Salaam wakati wa Mafunzo kwa Wanachama wa Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoa wa Dar es Salaam (DCPC) kuhusu Usambazaji na Matumizi ya Matokeo ya Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 yaliyoandaliwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Mtakwimu Mkuu kutoka NBS Elinzuu Nikodem amesema Utafiti huo umefanyika nchi nzima ikiwemo na Zanzibar.
Amesema Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa Mwaka 2022 (DHS-MIS 2022) ulilenga kutoa takwimu za kufuatilia na kutathmini hali ya afya ya watu nchini Tanzania.
Aidha ameongeza kuwa Utafiti wa DHS-MIS wa Mwaka 2022 ni wa saba katika mfululizo wa tafiti za kitaifa za kidemografia na afya zilizowahi kufanyika nchini Tanzania tangu mwaka 1991-92.
‘’Lengo la Utafiti huu ni kupata taarifa muhimu kuhusu kiwango cha uzazi, ndoa, kujamiiana, upendeleo wa kuzaa, ufahamu na matumizi ya njia za uzazi wa mpango, unyonyeshaji watoto wadogo, lishe, vifo vya watoto wadogo na vifo vitokanavyo na uzazi,
‘’ Huduma wakati wa ujauzito na huduma za watoto, malaria, na taarifa nyingine zinazohusu afya, pamoja na kiwango cha malaria kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano’’amesema Nikodem



Discussion about this post