NA ANDREW CHALE
KATIBU wa Siasa na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam, Ally Bananga amesema ni muhimu kusaidia jamii hususani kundi la watoto yatima na wale wenye uhitaji maalum kwa kuwa hakuna mzazi anayejua kesho yake itakavyokuwa..
Amesema ni muhimu kuendeleza utamaduni huo ndani ya jamii kwa kuwa mzazi anaweza kufurahia kuwa na mtoto au watoto wake sasa hivi lakini hajui yajayo ambapo anaweza kufariki dunia na kuwaacha yatima
Bananga ameyasema hayo Aprili 8,2024 mkoani Dar es Salaam wakati wa hafla maalum ya utoaji wa msaada kwa watoto yatima wa Kituo cha Mwandaliwa Orphanage Cente iliyoandaliwa na Taasisi ya Hitinas Foundation.
“Ukimsaidia mtoto yatima unaweka hazina nzuri mbele ya Mwenyezi Mungu, ambayo itakusaidia wewe au kizazi chako katika siku zijazo.
‘’Hongereni sana. (Hayati) Mzee Ali Hassan Mwinyi Rais wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesema (katika maisha yako) jiandae uwe hadithi nzuri huko mbeleni kwa hiyo mlichofanya Hitinas Foundation kupitia Mkurugenzi, nimefurahia sana, kwa sababu futari hii ya leo tumekula na wanaostahili kabisa”amesema Bananga
Bananga ameongeza kuwa milango ya CCM Mkoa wa Dar es Salaam ipo wazi na wako tayari kutoa ushirikiano watakaouhitaji ili kuwafanya watoto hao kuishi katika mazingira kama walivyo watoto wengine kwenye familia zao.
‘’Msikwazike wakati mnafanya mambo yenu,kwa haya ya kusaidia jamii njooni, kwa maana sisi wote nyumbani kwetu tuna mayatima watarajiwa leo tupo mambo yanaenda sawa sawa lakini kesho hatupo”amesisitiza Bananga’’
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Hinatas Foundation, Ayshat Sanya amesema walidhamiria kufutarisha watoto 105 wa kituo hicho ikiwemo kukusanya fedha kwa ajili ya kuwanunulia mahitaji mengine kama nguo na viatu vya kusherehekea sikukuu ya Eid.
.‘’Tunaishukuru jamii yetu, sisi ni taasisi inayosaidia jamii na asilimia 100 ni taasisi isiyojitengenezea faida na tumeweza kupata Tsh. Mililioni . tatu za nguo za Eid, ambapo tutanunua na kuwasilisha kituoni.
‘’Kituo cha Mwandaliwa leo ni mara ya kwanza tumeanza nao na tumeahidi kuendelea kuwashika mkono lakini tumeshafanya hivi na kituo kingine cha Al Madina na tutaendelea kushirikiana na vituo vingine pia’’ amesema Sanya
Naye Mlezi wa Mwandaliwa Orphanage Center ambaye pia ni Afisa, Elimu wa kituo hicho, Omary Daudi ameushukuru uongozi wa Hinatas Foundation kwa kuwaunga mkono katika kusaidia watoto hao.
”Watoto wamefurahi mno kwa tukio hili,lakini tunapoondoka hapa bado tuna mahitaji mengine mbalimbalii kama vyakula, sare za shule, sasa tuna usafiri changamoto ni fedha kwa ajili ya mafuta ya kuweka hivyo tunapenda kuona wadau mbalimbali wakiendelea kujitokeza kutusaidia” amebainisha Daudi.
Aidha, amebainisha kuwa, kituo hicho kina jumla ya watoto 105 kati yao wa kike ni 50 na wa kiume ni 55.




Discussion about this post