NA MWANDISHI WETU
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam imemuamuru Makamu Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi Joseph Roman Selasini kumuomba radhi James Mbatia ikiwepo kumlipa fidia ya kiasi cha Sh.Milioni 80.
Uamuzi huo wa Mahakama umetolewa Mei 2,2024 na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama hiyo Aron Lyamuya katika shauri la madai namba 87 la mwaka 2023 lililofunguliwa na James Mbatia dhidi ya Joseph Selasini.
Mbali na hilo lakini pia mahakama hiyo imeeleza kuwa maneno aliyotamka Joseph Selasini dhidi ya James Mbatia yalikuwa ya udhalilishaji na viashiria vya jinai kwa sababu yalikuwa yanahusu tuhuma za rushwa.
Hata hivyo Mahakama hiyo imemzuia Joseph Selasini au mtu yeyote kutoa maneno ya udhalilishaji dhidi ya James Francis Mbatia.
Uamuzi wa mahakama hiyo umetolewa baada ya James Mbatia kulalamikia kuhusu kauli iliyotolewa na Joseph Selasini katika kikao cha ndani kilichofanyika eneo la Mlango Mmoja Kata ya Nyasho Mkoa wa Mara kuwa alipokea fedha kutoka kwa Susan Masele kiasi cha Sh.Milioni 70 na Joyce Sokombi Sh.Milioni 30 ili waweze kuteuliwa kuwa wabunge wa viti maalum.
Hivyo Mbatia aliiomba kwanza aombwe radhi kwa kuchafuliwa, na pili aweze kulipwa fidia ya Sh Milioni 500, na mahakama itoe amri ya zuio kwa mtu yoyote au kwa Joseph Selasini kuendelea kumchafua ambapo pia aliomba gharama za kesi zilipwe na Joseph Selasini
Akizungumzia uamuzi huo Mei 3,2024 katika Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam Wakili wa James Mbatia,Hardson Mchau amesema shauri hilo ni la madai namba 87 la mwaka 2023 lililofunguliwa dhidi ya Joseph Selasini ambapo mahakama ilitoa maamuzi na kumpa ushindi mteja.
Amesema Mei 3,2024 wamefika katika Mahakama hiyo ya Kisutu kwa ajili ya kuwasilisha barua ya kuomba nakala ya uamuzi uliotolewa Mei 2,2024 na Mheshimiwa Hakimu Aron Lyamuya katika shauri hilo la madai namba 87 la 2023 ili waweze kuwasilisha maombi yao kwa ajili ya utekelezaji wa hukumu pamoja na gharama za shauri.
Amesema katika uamuzi huo, Mahakama iliamuru kwamba maneno aliyoongea Joseph Selasini huko Musoma yalikuwa ni maneno ya udhalilishaji na hivyo iliamuru aombe radhi aidha kwa kwenda Musoma alipotoa maneno hayo au kutoa kwenye ukurasa wa mbele wa gazeti linalosambazwa katika eneo kubwa la nchi.
‘’Mahakama ilienda mbali na kusema kwamba Joseph Roman Selasini aweze kumlipa mteja wangu James Mbatia kiasi cha Sh.Milioni 80 kama fidia kwa kumchafua,na pia Selasini anatakiwa kulipa gharama za shauri hivyo ndio maana tumewasilisha nyaraka hizi leo ili tuweze kutekeleza amri za mahakama”amesema Mchau.
Akizungumzia utekelezaji wa hukumu hiyo ,Mchau amebainisha kuwa kwa utekelezaji wa hukumu hiyo ulianza mara baada hukumu hiyo kutoka lakini kwa mujibu wa sheria ,ukomo wa utekelezaji wa hukumu ni miaka 12.
Kwa upande wa kukatiwa rufaa,Mchau amesema haki ya kukata rufaa ni haki ya kikatiba kwa kila upande na mtu yeyote ambaye anahisi hajaridhika na uamuzi kuna taratibu za ukataji wa rufaa.
‘’Je unatakiwa ujiulize hilo shauri lako unaweza kulikatia rufaa?kwa sababu rufaa sio haki ya moja kwa moja lazima ufuate taratibu na sio kila kesi inaweza kukatiwa rufaa kwani zingine rufaa zimezuiliwa kwa mujibu wa sheria.
‘’Kama upande wa pili wanaona hawajaridhika na wanahisi wana haki ya kukata rufaa wanaweza kukata rufaa kwenda Mahakama Kuu ya Tanzania”amefafanuwa Mchau.
Kwa upande wake James Mbatia amemshukuru Mchau kwa kazi kubwa aliyoifanya katika shauri hilo hadi maamuzi hayo yalipotolewa na mahakama.
‘’Ninachoweza kusema ni kwamba marafiki zangu wote kwa mapana yake kiini kikuu wakiwa ni watoto wa mama Tanzania wanaoamini katika kukuza na kuheshimu utu wa binadamu.
‘’Jaribio ovu la kutweza utu wangu limeshindwa,Mahakama imeongea,asante sana Mahakama”amesema Mbatia.




Discussion about this post