NA MWANDISHI WETU
WATANZANIA wametakiwa kufahamu kuwa Mahakama nchini zinatoa maamuzi kwa mujibu wa sheria na sio kwa misingi ya maelezo au maneno.
Ufafanuzi huo umetolewa na Wakili kutoka Kampuni ya Uwakili ya Mchau and Co.Advocates,Hardson Mchau wakati akizungumza na Bajeti Mei 6,2024 jijini Dar es Salaam kuhusu baadhi ya watu kulalamikia maamuzi ya mahakama yanayoupa ushindi upande wa pili na kueleza kuwa hawakutendewa haki.
Mchau amesema Mahakama ndio chombo kilichopewa Mamlaka ya Utendaji wa Haki Tanzania na kwa kuwa ndio chombo cha kutenda haki wanaamini kuwa Mahakama huwa inatenda haki.
Amesema mtu yeyote anayelalamika kuhusu mahakama kutotenda haki anatakiwa alalamike kwa misingi ya kisheria na sio misingi ya maelezo au maneno na anaposema hajatendewa haki ni lazima afafanuwe kuwa ni sheria gani haikufuatwa.
”Watu hawajui kuwa mahakama ni mahakama ya sheria,hapo ndio watu wanashindwa kujua tofauti ya haki na sheria.
”Hizi ni Mahakama za Sheria na Mahakama za Haki zipo ambazo zinaweza zisiangalie Sheria lakini kwa Tanzania Mahakama zetu ni Mahakama za Sheria na zinaitwa Court of Law.
”Sisi mahakama zetu ni mahakama za sheria na tunaangalia sheria inasemaje na ndio hivyo maamuzi yanaenda kutoka kwa mujibu wa sheria.”amesema Mchau
Mchau ambaye ni Mwanachama wa Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) tangu 2018,amefafanuwa kuwa haki nchini Tanzania inapatikana kwa mujibu wa sheria hivyo wakati mwingine mtu anahisi ana haki kumbe sheria imemnyima na ndio maana baadhi ya watu wanalalamika kwamba hawakutendewa haki.
”Sisi tunaamini kuwa Mahakama inatenda haki kwa sababu inafanya kazi kwa mujibu wa sheria na maamuzi yote ya Mahakama yanafanywa kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi.
”Kwa anayelalamika anatakiwa alalamike kwa misingi ya kisheria na sio misingi ya maelezo au maneno na unaposema hujatendewa haki ni lazima usema sheria gani haikufuatwa na sio kusema kwamba Mahakama haitendi haki”amebainisha Mchau.
Kwa upande wa kukata rufaa,Mchau ameongeza kuwa haki ya kukata rufaa ni haki ya kikatiba kwa kila upande na mtu yeyote ambaye anahisi hajaridhika na uamuzi kuna taratibu za ukataji wa rufaa.
”Je unatakiwa ujiulize hilo shauri lako unaweza kulikatia rufaa?kwa sababu rufaa sio haki ya moja kwa moja lazima ufuate taratibu na sio kila kesi inaweza kukatiwa rufaa kwani zingine rufaa zimezuiliwa kwa mujibu wa sheria”amebainisha Mchau
Amefafanuwa kuwa ikiwa upande wa pili wanaona hawajaridhika na wanahisi wana haki ya kukata rufaa wanaweza kukata rufaa.




Discussion about this post