NA BEATUS MAGANJA,ARUSHA .
MAMLAKA ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) imepokea vifaa vya aina mbalimbali kutoka kwa Marafiki wa Serengeti Uswisi vyenye thamani ya zaidi ya Sh.Milioni 40 ili vitumike katika kusaidia kuhifadhi na kulinda rasilimali za wanyamapori.
Hata hivyo ufadhili huo wa vifaa vya doria kwa TAWA umetolewa ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kuhifadhi na kulinda rasilimali za wanyamapori nchini ikiwa ni pamoja na udhibiti wa wanyamapori wakali na waharibifu,
Vifaa vilivyotolewa na Marafiki wa Serengeti Uswisi “Friends of Serengeti Switzerland” ni pamoja na mahema, mabegi ya kulalia “Sleeping bags” pamoja na Lita 2,120 za mafuta ya gari kwa ajili ya kusaidia shughuli za doria kwa Askari wa TAWA Kanda ya Kaskazini.
Akikabidhi vifaa hivyo Juni 9,2024 katika Ofisi za TAWA Kanda ya Kaskazini zilizopo jijini Arusha kwa niaba ya Bodi ya Marafiki wa Serengeti Uswisi, Suzan Shio amesema lengo na shabaha yao ni kusimamia uhifadhi wa mazingira na wanyamapori ili kuhakikisha Tanzania inakuwa katika hali yake ya uasili kwa ajili ya vizazi vya sasa na vijavyo.
“Tumekuwa tukifanya shughuli za ufadhili wa uhifadhi kwa miaka kadhaa nchini Tanzania, na kwa TAWA tumeanza zaidi ya miaka 10 iliyopita (tangu ikiwa Idara ya Wanyamapori) na hasa tulijikita kwenye ufadhili wa mafuta kwa ajili ya kuwasaidia askari kufanya doria” amesema Shio
Shio ameishukuru TAWA kwa ushirikiano inayoendelea kuutoa kwa wadau hao na kukiri kuwa ushirikiano huo umekuwa chachu ya kuwapa moyo wa kuendelea kuwafadhili.

Akizungumza mara baada ya kupokea vifaa hivyo, Kaimu Kamanda wa Uhifadhi TAWA Kanda ya Kaskazini Privatus Kasisi ameishukuru bodi ya Marafiki wa Serengeti kwa ufadhili huo ambao unalenga kuboresha usimamizi wa shughuli za uhifadhi na ulinzi wa rasilimali za wanyamapori hususani katika kukabiliana na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu katika Kanda hiyo.
“Sisi kama TAWA tunapenda kutoa shukrani zetu za dhati kwa bodi ya Marafiki wa Serengeti Uswisi ambao wamekuwa wakitusaidia misaada mbalimbali kwa ajili ya kusimamia uhifadhi na ulinzi wa rasilimali za wanyamapori kwa muda mrefu na wamekuwa wakitupa mafuta, mahema na viona mbali “binoculars’’
‘’Kanda ya Kaskazini inasimamia maeneo makubwa yanayounganisha mikoa minne ya Manyara, Arusha, Tanga na Kilimanjaro ambayo yamekuwa yakikumbwa na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu,hivyo kwa kupatiwa msaada huu hususani mahema yatawasaidia sana askari kufanya kazi zao ipasavyo hasa kwa kazi za dharura zinazojitokeza mara kwa mara na kuwalazimu kwenda maeneo ambayo hayana vituo vya kudumu vya askari’’ameongeza Kasisi.
Kasisi ameiomba bodi hiyo kuendelea kuisaidia TAWA hususani katika Kanda hiyo kwa kuwa wanasimamia maeneo makubwa yenye changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu na uhitaji bado ni mkubwa.




Discussion about this post