NA GOODLUCK HONGO
ZAO la Mkonge nchini Tanzana limeendelea kuwa neema kwa wakulima baada ya Serikali kuweka miundombinu bora na kusababisha kuongezeka kwa mahitaji yake kuliko uzalishaji.
Mbali na hilo lakini pia matumizi katika Sekta ya Ujenzi yamelifanya zao hilo kuwa adimu zaidi kuliko uzalishaji wake.
Akizungumza na Bajeti Communication mkoani Dar es Salaam wakati wa Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba,Mkuu wa Masoko kutoka Bodi ya Mkonge Tanzania David Maghali amesema kilo ya zao hilo kwa sasa ni kuanzia Sh.3000 lakini inategemea na daraja.
Amesema Serikali iligawa sana mbegu kwa wakulima ambao walipanda kwa wingi lakini kwa sasa mahitaji yamekuwa makubwa sana ambapo ulianza kupanda thamani tangu mwaka 2014.
‘’Kwa sasa Mkonge hakuna,na moja ya kitu kilichoongeza thamani ya Mkonge ni tasnia ya ujenzi,tunachojivunia sisi Mkonge haukidhi mahitaji ya watumiaji na tunataka watanzania wengi walime Mkonge na Kilimo hiki hakihitaji sana mbolea.
‘’Wenzetu wa Nchi za Afrika Magharibi kama Ginea-Conakry,Naigeria,Ghana zikiwemo na Saudi Arabia ndio watumiaji wakubwa wa Mkonge.
‘’Mkonge unatumika kutengeneza Gypsum(mapambo ya nyumba)Dashboard za magari,Kamba,mabegi na vingine vingi sana hali iliyolifanya kuongezeka kwa mahitaji yake zaidi duniani’’amesema Maghali
Hata hivyo Maghali amebainisha changamoto kubwa kwa wakulima kwa sasa ni mashine ya uchakataji zao hilo ambayo inauwezo wa kutenganisha jani na kamba zake.
‘’Kwa kuliona hilo Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imeamua kujenga vituo vya uchakataji Mkonge ambapo itanunua mashine kubwa yenye thamani ya zaidi ya Sh.Milioni 700 yenye uwezo wa kuchakata majani kuanzia hekari 10,000.
‘’Kituo cha kwanza kitaanza kujengwa Handeni mkoani Tanga na baadaye katika maeneo mengine ili kuondoa changamoto hiyo kwa sasa’’ameongeza Maghali

Machi 8,2023 Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) ilitangaza kuzalisha miche 500,000 ya zao la Mkonge kwa kutumia teknolojia ya chupa kutokana na ongezeko la mahitaji yake kitaifa.
,Mtafiti kutoka TARI-Mikocheni Margareth Lupembe alisema mbegu hizo zote zinazalishwa kwa njia ya chupa ndani ya maabara.
Amesema wao wamekuwa wakitumia teknolojia hiyo ya chupa maarufu kama Tissue Culture kwa muda mrefu ambapo mmea huzalishwa ndani ya chupa iliyokuwa na virutubisho vyote vinavyosaidia mmea kukua kama unavyokuwa nje.
“TARI-Mikocheni inatakiwa kuzalisha miche ya Mkonge 500,000 ifikapo Julai mwaka huu kwa ufadhili wa Serikali kupitia TARI Mlingano ili iweze kusambazwa kwa wakulima.
“TARI-Mikocheni sio tu tunazalisha miche ya Mkonge pekee au Nanasi lakini pia kuna mazao mengine kama migomba, mihogo na viazi vitamu ambayo yote tunazalisha kwa kutumia teknolojia ya chupa.”amesema Lupembe
Lupembe amefafanua kuwa uzalishaji wa mbegu bora kwa njia ya chupa ni tofauti na uzalishaji wa mbegu kwa njia zingine kama GMO hivyo ni muhimu wakulima na wadau wengine wa kilimo kujua hilo.
“Faida ya uzalishaji huu wa miche kwa njia ya chupa ni kwamba inatunza vinasaba,mimea yote inafafana kwa kuwa itatoka katika shina moja lakini pia ladha ni ile ile na mbegu zake zinaweza kupandwa kama kawaida”ameongeza Lupembe




Discussion about this post