NA MWANDISHI WETU
MAMLAKA ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (LATRA) itafunga mfumo maalum wa kufuatilia mwenendo wa gari kwa mabasi yanayotoa huduma ya usafiri ili kudhibiti ukatishaji wa njia zao.
Mbali na kufunga mfumo huo lakini pia ipo katika hatua za maandalizi ya kuweka mfumo wa tiketi zote za daladala kutumia mfumo wa kieletroni.
Kauli hiyo ya imetolewa Julai 7,2024 na Mkurugenzi wa Udhibiti Usafiri wa Barabara kutoka LATRA DCP Johansen Kahatano wakati wa Maonesho ya 48 ya Biashara ya Kimataifa Sabasaba yanayoeendelea mkoani Dar es salaam wakati akizungumza na Bajeti Communication.
Amesema wanaipongeza Serikali kwa uwekezaji wa barabara hasa za vijijini hivyo kumesaidia kuanzishwa kwa njia mpya nyingi na kufungwa kwa mfumo huo wa uthibiti katika daladala utasadia kuondoa hali hiyo ya ukatishaji wa njia kwa daladala.
‘’Hadi kufikia mwezi Desemba mfumo huo utakuwa umeshafungwa kwa daladala zote lakini pia tunaendelea na uwekaji wa mifumo ili tiketi zote za daladala zitolewe kwa njia ya mtandao.
‘’Lengo ni kuthibiti mapato ya Serikali,mmiliki wa gari na madereva akiwemo na Kondakta wake ambao wataajiriwa rasmi.
‘’Kwa upande wa Mabasi Yaendayo Kasi (BRT) wasafiri watatumia kadi kukata kitiketi zao kama ilivyo eneo la Feri jijini Dar es Salaam kwa watu wanaovuka kuelekea Kigamboni hivyo hakutakuwa na mfumo wa sasa kila atakayepanda itamlazimu kuwa kadi’’amesema Kahatano
Akizungumzia kuunganisha daladala au mabasi yanayotoka mkoa mwingine na Mkoa wa Dar es Salaam,Kahatano amefafanua kuwa wao wameona sio vibaya kuongeza kilomita tatu au mbili kwa maeneo yaliyopo karibu na yenye muingiliano mkubwa wa watu kuunganisha gari moja kwa kuwa Tanzania ni moja.
Kwa upande wa changamoto wanazokabiliana nazo kwa sasa ni ukatishaji wa safari kwa daladala na ndio maana wamekuja na mfumo huo wa kulifuatilia gari.
‘’Tunatoa wito kwa wananchi wote LATRA imeweka namba pembeni ya daladala na mabasi,hivyo wazitumie kuwapigia ili kutoa taarifa na wao watazifanyia kazi mara moja”amesema Kahatano




Discussion about this post