NA MWANDISHI WETU
TAASISI ya Utafiti wa Kilimo Tanzania (TARI) imegundua Mbegu mpya 16 za mazao ya Maharage, Korosho na Karanga zitakazoanza kutumika katika Msimu wa Kilimo wa mwaka 2024/2025.
Mbegu hizo mpya ambazo zimeidhinishwa na Kamati ya Taifa ya Mbegu (The National Seed Committee- NSC) zimefanyiwa utafiti na kugundulika kuwa zinasifa za kutoa mavuno mengi, kuwa na ukinzani dhidi ya magonjwa na kukomaa mapema.

Mbegu hizo ni pamoja na aina sita za Maharage ambazo ni TARIBEAN 6, TARIBEAN 7, TARIBEAN 8, TARIBEAN 9, TARIBEAN 10, TARIBEAN 11 na Karanga aina mbili ambazo ni TARIKA 1 na TARIKA 2.
Kwa upande wa Korosho jumla ya aina nane za mbengu bora za Korosho zimegunduliwa ambazo ni TARIKO-1, TARIKO-2, TARIKO-3, TARIKO-4, TARIKO-5, TARIKO-6, TARIKO-7 na TARIKO- 8.
Akizungumzia mbegu hizo Julai 13,2024, Mtaalamu wa Utafiti wa zao la Karanga Dkt. Happy Daud amesema Mbegu za Karanga zilizogunduliwa pamoja na sifa zingine ni za muda mfupi na hazishambuliwi na magonjwa tofauti na Mbegu za muda mfupi zilizopo ambazo hushambuliwa na magonjwa ya majani ambapo ugunduzi wa TARIKA1 na TARIKA 2 zinaenda kumsaidia mkulima.

Kwa upande wa zao la Korosho, Mtafiti wa zao hilo na Mkuu wa Idara ya Ugunduzi na Uzalishaji wa Mbegu Bora za Korosho kutoka Kituo cha TARI- Naliende Dadili Majune amesema Mbegu hizo mpya zina ukinzani wa ugonjwa wa Blaiti na sifa zote za uzaaji na ubora katika soko la Kimataifa.
Majune ameongeza kuwa ugunduzi huo utasaidia kupunguza matumizi ya viuatilifu vya ugonjwa wa Blaiti katika zao la Korosho.
Naye Mtafiti Kituo cha TARI-Uyole na Mratibu wa Maharage kitaifa Reinfrid Maganga amebainisha kuwa mbegu sita za Maharage zilizogunduliwa pamoja na kuwa na tija zaidi lakini zina sifa nyingine mbalimbali ambapo TARIBEAN 6 ni Maharage lishe yenye madini ya Zinki na Chuma kwa wingi zaidi kuliko aina zilizopo kwa sasa.
‘’TARIBEAN 7 ni jamii ya Rosekoko ikiwa na ukinzani mkubwa wa magonjwa ya Ndui na Madoa Pembe na TARIBEAN 8, ina sifa ya punje kubwa, inaiva haraka, tamu na inafanya vizuri sokoni.’’amesema Maganga
Huu ni mwendelezo wa matokeo ya tafiti na ugunduzi wa mbegu bora kutoka TARI ambayo ndiyo taasisi yenye dhamana ya kufanya na kuratibu Tafiti za Kilimo nchini, ambapo Mwaka 2023 ilisajili Mbegu mpya aina tano za Zabibu zilizoanza kutumika katika Msimu wa Kilimo wa 2023/2024.




Discussion about this post