NA MWANDISHI WETU,KATAVI
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema bajeti iliyopitishwa na Bunge kwa mwaka wa fedha 2024/25 ni Trilioni 1.25 kutoka Bilioni 460 miaka ya nyuma lengo likiwa ni kumuinua mkulima.
Rais Samia amebainisha kuwa kwa sasa Tanzania inahama kutoka katika kulima na kula na kuelekea katika Kilimo cha biashara.
Rais Samia ametoa kauli hiyo mkoani Katavi Julai 14,2024 wakati akihitimisha ziara yake kwa kutembelea maghala ya kuhifadhi chakula.
Amesema mahindi mpunga mbaazi na mazao yote ya chakula yamekuwa mazao ya biashara na ndio mazao yanayofanya vizuri katika kujenga uchumi.
”Tumedhamiria kukuza kilimo na tumeweza kuongeza bajeti ya Kilimo kutoka Sh.Bilioni 460 huko nyuma na mwaka huu bajeti ya Kilimo iliyopitishwa na Bunge ni Trilioni 1.25
”Lakini fedha hizi zinakwenda kwenye maeneo kadhaa ya kujenga skimu ya umwagiliaji maji,maeneo ya kukuza huduma za ugani na kama mnavyojua tunatoa mbolea ya ruzuku,Serikali inabeba nusu gharama na mwananchi unalipa nusu gharama ili kukuza uzalishaji zaidi na kuwa na mazao mengi zaidi.
”Tumeanza kufanya biashara na nchi jirani,na sasa hivi tunafanya biashara na Zambia wanachukua zaidi ya tani 600,000 kutoka Tanzania kwa sababu wao wamepata ukame,sasa lazima tukuze tija na uwezo wa maghala yetu ichukule chakula kingi zaidi.”amesema Rais Samia
Amebainisha kuwa kwa sasa wanajipanga ili waweze kufikia tani milioni tatu itakapofika mwaka 2030 kwa Tanzania yote iweze kuhifadhi tani milioni tatu.
‘’Jana nilitoa ruhusa Mkoa wa Katavi iwe Kanda inayojitegemea peke yake katika manunuzi ya nafaka na katika uhifadhi wa chakula na tujielekeze kwenye uzalishaji ili mkulima anufaike na Serikali inufaike na Taifa kwa ujumla linufaike”amesema Rais Samia
Aidha Rais Samia amebainisha kuwa Sh.Bilioni 14 zimetumika katika mradi huo na kwa sababu wameamua Katavi iwe Kanda inayojitegemea peke yake ni lazima waongeze uwezo wa kuhifadhi
”Kile kilio cha wakulima cha kudhulumiwa sifa ya mazao yake au grade ya mazao yake au uzito sasa hakipo tena
”Kuna mfumo mzuri wa mkulima wa kupima mazao yake na anaridhika na ni automatic na hauingii mkono wa mtu,unachokiweka ndicho kinachojiandika kwenye mizani”amefafanuwa Rais Samia
Rais Samia ameongeza kuwa wamekusudia kuipandisha NFRA kiutendeaji,kiteknolojia,kifedha na kuwataka wakulima kulima kwa wingi ili anayenunua kwa mkulima anunue kwa haki na vizuri na anayeongeza dhamani ya mazao aongeze vizuri akiwemo na anayeuza naye auze vizuri




Discussion about this post